Utenzi wa Daudi Pangoni
Kwa mwimbishaji. Kwa mtindo wa "Usiharibu." Utenzi wa Daudi, alipomkimbia Sauli akaingia pangoni.
57 1 Unifadhili, Baba yangu, unifadhili, kwa maana nafsi yangu inakukimbilia wewe; katika uvuli wa mbawa zako nitakimbilia hata dhoruba ziharibuzo zipite. 2 Namlilia Baba yangu, Aliye juu, Baba yetu anitimiziaye makusudi yake kwangu.
3 Atatuma toka mbinguni na kuniokoa; humkemea yule anikanyagaye mimi. Sela. Baba yangu atatuma upendo wake wa agano na uaminifu wake. 4 Nafsi yangu i katikati ya simba; nalala kati ya wale wapumuao moto — watu ambao meno yao ni mikuki na mishale, ndimi zao ni panga kali. 5 Utukuzwe, Baba yangu, juu ya mbingu! Utukufu wako uwe juu ya nchi yote!
6 Walitega wavu kwa hatua zangu; nafsi yangu ikainama. Walichimba shimo mbele yangu, lakini wao wenyewe wametumbukia ndani yake. Sela. 7 Moyo wangu ni thabiti, Baba yangu, moyo wangu ni thabiti! Nitaimba na kupiga mziki. 8 Amka, utukufu wangu! Amka, kinubi na zeze! Nitaiamsha alfajiri. 9 Nitakusifu kati ya watu, Ee Baba mwenye enzi; nitakuimbia kati ya mataifa. 10 Kwa maana upendo wako wa agano wafika mbinguni, uaminifu wako hata mawinguni. 11 Utukuzwe, Baba yangu, juu ya mbingu! Utukufu wako uwe juu ya nchi yote!