Hakuna Doa Kwako
Mwanamume amsifu mwanamke kiungo baada ya kiungo, amwita bibi-arusi wake na dada yake, asema hakuna dosari ndani yake. Yeye ni bustani iliyofungwa, chemchemi iliyotiwa muhuri, yake peke yake. Mwishoni yeye ajibu, akiuita upepo na kuifungua bustani hiyo mwenyewe.
4 1Tazama, wewe ni mzuri, mpenzi wangu, tazama, wewe ni mzuri! Macho yako ni kama ya njiwa nyuma ya utaji wako. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi washukao kwenye miteremko ya Gileadi. 2Meno yako ni kama kundi la kondoo waliokatwa manyoya karibuni, wakipanda kutoka kuoga, kila mmoja akizaa mapacha, wala hakuna hata mmoja aliyefiwa na mwanawe. 3Midomo yako ni kama uzi mwekundu, na kinywa chako ni cha kupendeza. Mashavu yako ni kama vipande viwili vya komamanga nyuma ya utaji wako. 4Shingo yako ni kama mnara wa Daudi, uliojengwa kwa safu za mawe; juu yake hutundikwa ngao 1,000, kila moja ni ngao ya shujaa. 5Maziwa yako mawili ni kama wana-paa wawili, mapacha wa paa, wakila katika mahali penye maua ya yungiyungi. 6Hata siku ipumzikapo na vivuli vikimbiapo, nitakwenda mlima wa manemane na kilima cha ubani. 7Wewe u mzuri kabisa, mpenzi wangu; hakuna doa kwako.
8Njoo pamoja nami kutoka Lebanoni, bibi arusi wangu; njoo pamoja nami kutoka Lebanoni. Tazama chini kutoka kilele cha Amana, kutoka kilele cha Seniri na Hermoni, kutoka mapango ya simba, kutoka milima ya makao ya chui. 9Umeuteka moyo wangu, dada yangu, bibi arusi wangu; umeuteka moyo wangu kwa mtazamo mmoja wa macho yako, kwa kito kimoja cha mkufu wako. 10Jinsi upendo wako ulivyo mzuri, dada yangu, bibi arusi wangu! Upendo wako ni bora zaidi kuliko divai, na harufu nzuri ya mafuta yako kuliko kiungo chochote! 11Midomo yako yadondoza asali safi, bibi arusi wangu; asali na maziwa vi chini ya ulimi wako, na harufu nzuri ya mavazi yako ni kama harufu nzuri ya Lebanoni.
12Bustani iliyofungwa ndiyo dada yangu, bibi arusi wangu, chemchemi iliyofungwa, kisima kilichotiwa muhuri. 13Matawi yako ni bustani ya mikomamanga yenye matunda bora kabisa, hina pamoja na nardo, 14nardo na zafarani, mchai na mdalasini, pamoja na kila mti wa ubani, manemane na udi, pamoja na viungo vyote bora kabisa. a a v14 Mchai ni tete lenye harufu nzuri litumiwalo kama kiungo. 15Wewe u chemchemi ya bustani, kisima cha maji yaliyo hai, na vijito vitiririkavyo kutoka Lebanoni. 16Amka, upepo wa kaskazini, na uje, upepo wa kusini! Vuma juu ya bustani yangu, ili viungo vyake vitiririke. Mpenzi wangu na aingie katika bustani yake, na kula matunda yake bora kabisa.