Siku ya Arusi ya Mfalme
Mwanamke amtafuta katika mji wa giza yule ampendaye, awauliza walinzi, kisha ampata na hamwachi mpaka amlete nyumbani kwa mama yake. Kisha sauti nyingine zatazama gari la Sulemani likikaribia likiwa na ulinzi, mfalme akiwa amevikwa taji siku ya arusi yake.
3 1Kitandani mwangu usiku kucha nilimtafuta yeye ambaye nafsi yangu impenda; nilimtafuta, lakini sikumwona. 2Sasa nitaondoka na kuuzunguka mji, katika njia na viwanja; nitamtafuta yeye ambaye nafsi yangu impenda. Nilimtafuta, lakini sikumwona. 3Walinzi wakanikuta walipokuwa wakizunguka mji. "Je, mmemwona yeye ambaye nafsi yangu impenda?" 4Nilikuwa nimewapita kidogo tu ndipo nikamwona yeye ambaye nafsi yangu impenda. Nikamshika wala nisimwache aende zake hata nilipomleta nyumbani mwa mama yangu, ndani ya chumba cha yeye aliyenichukua mimba. 5Nawaapisha, enyi binti za Yerusalemu, kwa paa na kwa ayala wa kondeni: msiiamshe wala kuisisimua mapenzi hata itakapopenda yenyewe.
6Ni nani huyu apandaye kutoka jangwani kama nguzo za moshi, akifukizwa manemane na uvumba, pamoja na poda zote zenye harufu nzuri za mfanyabiashara? 7Tazama—ni gari lake mwenyewe Sulemani, likizungukwa na mashujaa sitini, katika mashujaa wa Israeli, 8wote wameshika panga, wamezoezwa vita, kila mmoja ana upanga wake pajani pake, dhidi ya hofu ya usiku. 9Mfalme Sulemani alijifanyia gari kwa mbao za Lebanoni. 10Aliyafanya mategemeo yake kwa fedha, mgongo wake kwa dhahabu, kiti chake kwa rangi ya zambarau; ndani yake kilinakshiwa kwa upendo na binti za Yerusalemu. 11Tokeni nje, enyi binti za Sayuni, mkamtazame Mfalme Sulemani, akiwa amevaa taji aliyomvika mama yake siku ya arusi yake, siku ya furaha ya moyo wake.