Kilio cha Daudi kwa Wokovu
Shigayoni ya Daudi, aliyomwimbia Baba yetu kwa habari ya Kushi, Mbenyamini.
7 1 Ee Baba yangu, kwako nakimbilia; niokoe na wote wanaonifuatia, unikomboe, 2 asije akanirarua kama simba, akinipasua vipande vipande wala hakuna wa kuniokoa. 3 Ee Baba yangu, kama nimetenda hili — kama kuna uovu mikononi mwangu, 4 kama nimemlipa mwenzangu kwa ubaya, au nimemteka nyara adui yangu bila sababu — 5 basi adui na anifuatie na kunipata, na akanyage uhai wangu chini, na alaze heshima yangu mavumbini. Sela
6 Ondoka, Baba yangu, katika hasira yako; inuka juu ya ghadhabu ya adui zangu; niamkie mimi — umeamuru hukumu. 7 Kusanyiko la mataifa na likuzunguke; keti mahali pa juu juu yao. 8 Baba yetu huyahukumu mataifa. Nihukumie haki, Baba yangu, kwa kadiri ya haki yangu na kwa kadiri ya ukamilifu ulio ndani yangu. 9 Ukomeshe ubaya wa waovu, bali umtegemeze mwenye haki — wewe uchunguzaye nia na mioyo, Ee Baba mwenye haki. 10 Ngao yangu ni Baba yangu, awaokoaye wanyofu wa moyo. 11 Baba yetu ni mwamuzi mwenye haki, Mungu aliye na hasira kila siku. 12 Mtu asipotubu, Baba yetu atanoa upanga wake; ameuvuta upinde wake na kuufanya tayari. 13 Ameviandaa vyombo vyake vya kufisha; azifanya mishale yake kuwa mienge ya moto. 14 Tazama jinsi mtu mwovu alivyo na mimba ya uovu; hutunga taabu na kuzaa uongo. 15 Huchimba shimo na kulifukua, lakini huanguka katika shimo alilolitengeneza. 16 Taabu yake humrudia juu ya kichwa chake mwenyewe; jeuri yake humshukia juu ya utosi wake mwenyewe. 17 Nitamshukuru Baba yangu kwa ajili ya haki yake, nami nitaliimbia sifa jina la Baba yangu, Aliye Juu Sana.