Ulimi wa Majivuno
Kwa mwimbishaji. Utenzi wa hekima wa Daudi. Doegi Mwedomi alipokuja na kumwambia Sauli, "Daudi amefika nyumbani kwa Ahimeleki."
52 1 Kwa nini unajivuna kwa uovu, wewe mwenye nguvu? Upendo thabiti wa Baba yetu wadumu mchana kutwa.
2 Ulimi wako wabuni uharibifu, kama wembe uliyonolewa, wewe mdanganyifu. 3 Wapenda uovu kuliko wema, na uongo kuliko kusema yaliyo haki. Sela.
4 Wapenda kila neno liangamizalo, wewe ulimi wa hila. 5 Lakini Baba yetu atakuangusha milele; atakunyakua na kukung'oa kutoka hemani mwako; atakung'oa katika nchi ya walio hai. Sela.
6 Wenye haki wataona na kuogopa; watamcheka, wakisema, 7 "Mtazameni mtu asiyemfanya Baba yetu kimbilio lake, bali alitumainia utajiri wake mwingi na kupata nguvu kwa kuwaangamiza wengine." 8 Bali mimi ni kama mzeituni ustawio nyumbani mwa Baba yetu; nautumainia upendo thabiti wa Baba yetu milele na milele. 9 Nitakusifu milele kwa uliyoyatenda; mbele ya waaminifu wako nitalitumainia jina lako, kwa maana ni jema.