Waovu na Njia Zao
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi, mtumishi wa Baba yetu.
36 1 Uovu humwambia mtu mbaya ndani sana ya moyo wake; hakuna kumcha Baba yetu mbele ya macho yake.
2 Kwa maana hujipendekeza machoni pake mwenyewe kiasi kwamba hawezi kuutambua dhambi yake wala kuichukia. 3 Maneno ya kinywa chake ni uovu na hila; ameacha kutenda kwa hekima na kufanya mema. 4 Hata kitandani mwake hupanga hila; hujiweka katika njia isiyo njema; hakatai lililo baya.
5 Baba yetu, upendo wako thabiti wa agano hufika mbinguni, uaminifu wako hufika mawinguni. 6 Haki yako ni kama milima mikubwa, hukumu zako ni kama vilindi vikuu; wewe huwaokoa watu na wanyama pia, Baba yetu. 7 Jinsi ulivyo wa thamani upendo wako thabiti wa agano, Baba yetu! Watu wote hukimbilia hifadhi chini ya uvuli wa mbawa zako. 8 Hushiba kwa wingi wa nyumba yako, nawe huwanywesha katika mto wa furaha zako. 9 Kwa maana kwako wewe iko chemchemi ya uzima; katika nuru yako twaona nuru.
10 Uendeleze upendo wako thabiti wa agano kwa wale wakujuao, na haki yako kwa wanyoofu wa moyo. 11 Usiache mguu wa mwenye kiburi unikanyage, wala mkono wa mtu mbaya usinifukuze. 12 Hapo watenda maovu wameanguka; wametupwa chini, hawawezi kuinuka.