Unipiganie, Baba yangu
Ya Daudi.
35 1 Ushindane, Baba yangu, na wale wanaoshindana nami; upigane na wale wanaopigana nami.
2 Twaa ngao na kigao, uinuke unisaidie.
3 Ufute mkuki na fumo dhidi ya wanaonifuatia; uiambie nafsi yangu, "Mimi ni wokovu wako."
4 Waaibike na kutahayarika wanaotafuta uhai wangu; warudishwe nyuma na kufedheheshwa wanaonipangia mabaya. 5 Wawe kama makapi mbele ya upepo, malaika wa Baba yetu akiwafukuza. 6 Njia yao na iwe giza na utelezi, malaika wa Baba yetu akiwafuatia.
7 Kwa maana bila sababu wameuficha wavu wao kwa ajili yangu; bila sababu wamenichimbia shimo kwa uhai wangu. 8 Uharibifu na umjie ghafula bila kutazamia; wavu aliouficha na umnase; katika uharibifu huohuo na aanguke.
9 Ndipo nafsi yangu itakapofurahi katika Baba yangu; itashangilia katika wokovu wake. 10 Mifupa yangu yote itasema, "Baba yangu, ni nani aliye kama wewe, uokoaye maskini kutoka kwa aliye na nguvu kuliko yeye, maskini na mhitaji kutoka kwa amwibiaye?"
11 Mashahidi wenye nia mbaya wanainuka; wananiuliza mambo nisiyoyajua. 12 Wananilipa mabaya kwa mema; nafsi yangu imeachwa ukiwa. 13 Lakini mimi, walipokuwa wagonjwa, nilivaa nguo za maombolezo; nilijinyenyekeza kwa kufunga, na maombi yangu yakawa yakinirudia moyoni mwangu. a a v13 "Maombi yangu yakawa yakinirudia moyoni mwangu" maana yake si dhahiri; huenda ikamaanisha kwamba maombi ya Daudi yalikuwa ya kweli lakini hayakujibiwa. 14 Nilikwenda huku na huko kana kwamba ninamwombolezea rafiki yangu au ndugu yangu; niliinama chini kwa maombolezo, kama amliliaye mama yake. 15 Lakini nilipojikwaa walifurahi na kukusanyika pamoja; washambuliaji nisiowajua walikusanyika dhidi yangu, wakinirarua bila kukoma. 16 Kama wenye dhihaka wasiomcha Mungu katika karamu, walinisagia meno yao.
17 Ee Baba yangu Mwenye Enzi, hata lini utatazama tu? Uokoe nafsi yangu na maangamizi yao, uhai wangu wa pekee na simba. 18 Nitakushukuru katika kusanyiko kuu; miongoni mwa umati mkubwa nitakusifu. 19 Adui zangu wadanganyifu wasinishangilie, wala wanaonichukia bila sababu wasikonyeze jicho. b b v19 Yesu aliyatumia maneno haya juu yake mwenyewe — wale waliomchukia "bila sababu" — kama chuki ambayo ulimwengu ulimwonyesha njiani kuelekea msalabani (Yohana 15:25). 20 Kwa maana hawanenei amani, bali dhidi ya watu watulivu wa nchi hupanga hila za udanganyifu. 21 Wanapanua vinywa vyao dhidi yangu; wanasema, "Aha! Aha! Macho yetu wenyewe yameona!"
22 Umeona, Baba yangu; usinyamaze. Ee Baba yangu Mwenye Enzi, usiwe mbali nami. 23 Amka, ujiamshe, uitetee haki yangu, kwa ajili ya shauri langu, Ee Baba yangu Mwenye Enzi! 24 Unihukumie haki, Baba yangu, sawasawa na haki yako, wala usiwaache wanishangilie. 25 Wasiseme mioyoni mwao, "Aha, ndivyo tulivyotaka!" Wasiseme, "Tumemmeza."
26 Waaibike na kufedheheshwa pamoja wale wanaofurahia msiba wangu; wavikwe aibu na fedheha wale wanaojigamba juu yangu. 27 Wale wapendezwao na kutetewa kwa haki yangu na wapige kelele za furaha na wafurahi; nao waseme daima, "Baba yetu ni mkuu, apendezwaye na fanaka ya mtumishi wake!"
28 Ndipo ulimi wangu utakaposimulia haki yako, na sifa zako mchana kutwa.