Onjeni Mwone
Zaburi ya Daudi, alipojifanya mwendawazimu mbele ya Abimeleki, aliyemfukuza, naye akaenda zake.
34 1 Nitamhimidi Baba yetu nyakati zote; sifa zake zitakuwa daima midomoni mwangu.
2 Nafsi yangu itajisifu katika Baba yetu; wanyenyekevu wasikie na kufurahi. 3 Mtukuzeni Baba yetu pamoja nami; na tuliadhimishe jina lake pamoja.
4 Nalimtafuta Baba yetu, naye akanijibu; akaniokoa na hofu zangu zote. 5 Wamtazamao hung'aa kwa furaha; nyuso zao hazitaona haya kamwe. 6 Maskini huyu aliita, naye Baba yetu akamsikia; akamwokoa katika taabu zake zote. 7 Malaika wa Baba yetu hufanya kituo akiwazunguka wamchao, naye huwaokoa.
8 Onjeni mwone ya kuwa Baba yetu ni mwema; heri mtu anayemkimbilia. 9 Mcheni Baba yetu, enyi watakatifu wake, maana wamchao hawapungukiwi na kitu. 10 Wana simba hupata njaa na kupungukiwa, bali wamtafutao Baba yetu hawatakosa kitu chema chochote.
11 Njooni, watoto, nisikilizeni; nitawafundisha kumcha Baba yetu. 12 Ni nani mtu anayetaka uzima, apendaye siku nyingi njema? 13 Uuzuie ulimi wako na uovu, na midomo yako isiseme hila. 14 Jiepushe na uovu, ukatende mema; tafuta amani na kuifuatia.
15 Macho ya Baba yetu yako kwa wenye haki, na masikio yake yako wazi kwa kilio chao. 16 Uso wa Baba yetu u kinyume cha watendao maovu, ili kukatilia mbali kumbukumbu lao duniani. 17 Wenye haki hulia, naye Baba yetu husikia; huwaokoa katika taabu zao zote. 18 Baba yetu yu karibu na waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho.
19 Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini Baba yetu humwokoa kila mmoja na hayo yote. 20 Baba yetu huihifadhi mifupa yote ya mwenye haki; hakuna hata mmoja wao unaovunjika.
21 Uovu utamwua mtu mbaya, na wamchukiao mwenye haki watahukumiwa. 22 Baba yetu huikomboa nafsi ya watumishi wake; hakuna anayemkimbilia atakayehukumiwa.