Uumbaji Wanena
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
19 1 Mbingu zauhubiri utukufu wa Baba yetu; anga latangaza kazi ya mikono yake. 2 Siku baada ya siku hufoka maneno; usiku baada ya usiku hufunua maarifa. 3 Hakuna usemi, hakuna maneno — sauti yao haisikiki kamwe. 4 Lakini sauti yao huenea katika dunia yote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. Katika mbingu ameweka hema kwa ajili ya jua, 5 nalo ni kama bwana arusi atokaye chumbani mwake, kama shujaa afurahiaye kupiga mbio zake. 6 Latokea upande mmoja wa mbingu, na mzunguko wake wafika upande wa pili; wala hakuna kilichofichika na joto lake.
7 Sheria ya Baba yetu ni kamilifu, huiburudisha nafsi; ushuhuda wa Baba yetu ni wa kuaminika, humpa mjinga hekima. 8 Maagizo ya Baba yetu ni ya adili, huufurahisha moyo; amri ya Baba yetu ni angavu, huyatia macho nuru. 9 Kicho cha Baba yetu ni safi, kidumucho milele; hukumu za Baba yetu ni za kweli, tena zote pamoja ni za haki. 10 Zinatamanika kuliko dhahabu, naam, kuliko dhahabu iliyo safi kabisa; ni tamu kuliko asali, kuliko asali itokayo katika sega. 11 Kwazo mtumishi wako huonywa; katika kuzishika kuna thawabu kubwa.
12 Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake mwenyewe? Unitakase na makosa yangu yaliyofichika. 13 Pia mzuie mtumishi wako na dhambi za kusudi; zisinitawale mimi. Ndipo nitakapokuwa mkamilifu, wala sitakuwa na hatia ya kosa kuu.
14 Maneno ya kinywa changu na mawazo ya moyo wangu yakubalike mbele zako, Ee Baba yangu, mwamba wangu na mkombozi wangu.