Viumbe Vyote, Msifuni Yeye
148 1 Haleluya! Msifuni Baba yetu kutoka mbinguni; msifuni katika mahali palipo juu. 2 Msifuni, enyi malaika wake wote; msifuni, enyi majeshi yake yote. 3 Msifuni, jua na mwezi; msifuni, enyi nyota zote zing'aazo. 4 Msifuni, enyi mbingu zilizo juu sana, na enyi maji yaliyo juu ya mbingu. 5 Na vilisifu jina la Baba yetu, kwa maana aliamuru, navyo vikaumbwa. 6 Akaviimarisha milele na milele; akatoa amri isiyopita.
7 Msifuni Baba yetu kutoka nchini, enyi viumbe vya baharini na vilindi vyote vya bahari, 8 moto na mvua ya mawe, theluji na ukungu, upepo wa dhoruba utimizao neno lake, 9 milima na vilima vyote, miti ya matunda na mierezi yote, 10 wanyama wa mwitu na wanyama wote wa kufugwa, vitambaavyo na ndege warukao, 11 wafalme wa dunia na watu wote, wakuu na watawala wote wa dunia, 12 vijana waume na vijana wake pia, wazee na watoto.
13 Na wasifu jina la Baba yetu, kwa maana jina lake peke yake limetukuka; fahari yake i juu ya nchi na mbingu. 14 Amewainulia watu wake nguvu, sifa kwa waaminifu wake wote, kwa ajili ya watu wa Israeli walio karibu naye. Haleluya!