Baba yangu, Mfalme wangu
Zaburi ya sifa. Ya Daudi.
145 1 Nitakutukuza wewe, Baba yangu, Mfalme wangu, nami nitalibariki jina lako milele na milele.
2 Kila siku nitakubariki wewe, nami nitalisifu jina lako milele na milele. 3 Baba yetu ni mkuu, na anayestahili kusifiwa sana; ukuu wake hakuna awezaye kuupima.
4 Kizazi kimoja kitasifia matendo yako kwa kizazi kingine, na kitazitangaza kazi zako zenye nguvu. 5 Nitatafakari fahari tukufu ya enzi yako na juu ya matendo yako ya ajabu. 6 Watasimulia nguvu za matendo yako ya kutisha, nami nitautangaza ukuu wako. 7 Watafurika kwa kumbukumbu ya wema wako mwingi, na wataimba kwa furaha juu ya haki yako.
8 Baba yetu ni mwenye neema na amejaa huruma, si mwepesi wa hasira na mkuu katika upendo wa agano. 9 Baba yetu ni mwema kwa wote, na moyo wake wa huruma unakaa juu ya vyote alivyovifanya. 10 Kazi zako zote zitakushukuru, Baba yetu, na waaminifu wako watakubariki. 11 Watanena utukufu wa ufalme wako na kusimulia nguvu zako, 12 ili kuwajulisha wanadamu matendo yako yenye nguvu, na fahari tukufu ya ufalme wako. 13 Ufalme wako ni ufalme wa milele, na mamlaka yako yadumu vizazi vyote. Baba yetu ni mwaminifu katika maneno yake yote, na mwenye neema katika kazi zake zote.
14 Baba yetu huwategemeza wote wanaoanguka, na huwainua wote walioinama. 15 Macho ya wote yanatazama kwako wewe, nawe huwapa chakula chao kwa wakati wake. 16 Waufumbua mkono wako na kuyashibisha matakwa ya kila kilicho hai.
17 Baba yetu ni mwenye haki katika njia zake zote na mwaminifu katika kazi zake zote. 18 Baba yetu yu karibu na wote waitao kwake, na wote wamwitao kwa kweli. 19 Hutimiza matakwa ya wale wamchao yeye; husikia kilio chao, naye huwaokoa. 20 Baba yetu huwalinda wote wampendao yeye, bali waovu wote atawaangamiza.
21 Kinywa changu kitanena sifa za Baba yetu; kila kilicho hai na kilibariki jina lake takatifu milele na milele.