Mwamba Wangu, Kimbilio Langu
Zaburi ya Daudi.
144 1 Ahimidiwe Baba yangu, mwamba wangu, aifundishaye mikono yangu vita, na vidole vyangu kupigana— 2 upendo wangu thabiti na ngome yangu, boma langu na mwokozi wangu, ngao yangu ninayemkimbilia, awatiishaye watu chini yangu.
3 Baba yangu, mwanadamu ni nini hata umjali, binadamu hata umfikirie? 4 Mwanadamu ni kama pumzi; siku zake ni kama kivuli kipitacho.
5 Baba yangu, inamisha mbingu zako ushuke; gusa milima, nayo itatoa moshi. 6 Piga umeme wako, uwatawanye wao; peleka mishale yako, uwavuruge. 7 Nyoosha mkono wako toka juu; uniokoe mimi, na uniponye kutoka maji makuu, kutoka mikononi mwa wageni, 8 ambao vinywa vyao hunena uongo, na mkono wao wa kuume huapa kwa uongo.
9 Baba yangu, nitakuimbia wimbo mpya; kwa kinubi cha nyuzi kumi nitakuimbia sifa, 10 wewe uwapaye wafalme ushindi, umwokoaye Daudi mtumishi wako kutoka upanga mkali.
11 Uniokoe mimi, na uniponye kutoka mikononi mwa wageni, ambao vinywa vyao hunena uongo, na mkono wao wa kuume huapa kwa uongo.
12 Ndipo wana wetu watakuwa kama mimea iliyokua vizuri katika ujana wao, binti zetu kama nguzo za pembeni zilizonakshiwa kwa ajili ya jumba la kifalme. 13 Ghala zetu zitakuwa zimejaa, zikitoa mazao ya kila aina; makundi yetu yataongezeka kwa maelfu, kwa makumi elfu mashambani mwetu; 14 ng'ombe wetu wenye mimba, pasipo kuta kubomolewa, wala kwenda utumwani, wala kilio cha taabu katika njia zetu. 15 Heri watu ambao mambo kama hayo ni yao; heri watu ambao Baba yetu ndiye wao.