Njia Ipitayo Samaria
4 1 Basi Yesu alipojua kwamba Mafarisayo wamesikia ya kuwa yeye anafanya na kubatiza wanafunzi wengi kuliko Yohana 2 (ingawa Yesu mwenyewe hakuwa akibatiza, bali wanafunzi wake), 3 aliondoka Uyahudi akarudi Galilaya. 4 Na ilimpasa kupita katikati ya Samaria. 5 Basi akafika katika mji wa Samaria uitwao Sikari, karibu na lile shamba Yakobo alilompa mwanawe Yusufu. 6 Kisima cha Yakobo kilikuwako hapo. Naye Yesu, akiwa amechoka kwa safari, akaketi hivi kando ya kisima—yapata saa sita mchana. a a v6 Kwa kuhesabu tangu macheo ya jua, saa sita ni yapata adhuhuri.
7 Mwanamke mmoja Msamaria akaja kuteka maji. Yesu akamwambia, "Nipe maji ninywe."
8 (Kwa maana wanafunzi wake walikuwa wamekwenda mjini kununua chakula.)
9 Yule mwanamke Msamaria akamwambia, "Wewe u Myahudi; yakuwaje wataka kunywa kwangu mimi niliye mwanamke Msamaria?" (Kwa maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.)
10 Yesu akajibu akamwambia, "Kama ungalijua karama ya Baba yetu, naye ni nani akuambiaye, 'Nipe maji ninywe,' ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai."
11 Yule mwanamke akamwambia, "Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu. Basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? 12 Je, wewe u mkuu kuliko baba yetu Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akakinywea, na wanawe, na mifugo yake?"
13 Yesu akajibu akamwambia, "Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; 14 lakini yeye atakayekunywa maji nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji yabubujikayo hata uzima wa milele."
15 Yule mwanamke akamwambia, "Bwana, nipe maji hayo, nisipate kiu wala nisije hapa kuteka."
16 Yesu akamwambia, "Nenda ukamwite mumeo, uje naye hapa."
17 Yule mwanamke akajibu akasema, "Sina mume." Yesu akamwambia, "Umesema vema, 'Sina mume';
18 kwa maana umekuwa na waume watano, na huyu uliye naye sasa siye mumeo. Katika hilo umesema kweli."
19 Yule mwanamke akamwambia, "Bwana, naona ya kuwa u nabii. 20 Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi mwasema ya kwamba Yerusalemu ndipo mahali pawapasapo watu kuabudia."
21 Yesu akamwambia, "Mama, niamini, saa yaja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. 22 Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tunachokijua—kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi. 23 Lakini saa yaja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli—kwa maana Baba awatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu. 24 Baba ni roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli." b b v24 Katika fungu hili lote Yesu afundisha juu ya kumwabudu Baba; yeye ambaye asili yake ni roho ndiye Baba yuleyule awatafutaye waabuduo halisi.
25 Yule mwanamke akamwambia, "Najua ya kuwa Masihi—yule aitwaye Kristo—anakuja. Naye atakapokuja, atatuambia mambo yote."
26 Yesu akamwambia, "Mimi ndiye—nisemaye nawe."
27 Wakati huohuo wanafunzi wake wakaja, wakastaajabu kwa kuwa alikuwa akisema na mwanamke. Lakini hakuna aliyesema, "Wataka nini?" au, "Mbona wasema naye?" 28 Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, 29 "Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je, huyu siye Kristo?" 30 Wakatoka mjini, wakawa wakija kwake.
31 Wakati ule ule wanafunzi wake walikuwa wakimsihi, wakisema, "Rabi, ule chakula."
32 Naye akawaambia, "Mimi ninacho chakula cha kula msichokijua ninyi."
33 Basi wanafunzi wakaambiana, "Je, kuna mtu aliyemletea kitu ale?"
34 Yesu akawaambia, "Chakula changu ndicho hiki, niyafanye mapenzi yake yeye aliyenituma, na kuikamilisha kazi yake. 35 Je, ninyi hamsemi, 'Bado miezi minne, ndipo mavuno yaja'? Tazameni, nawaambia: inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. 36 Naye avunaye tayari apokea ujira, na kukusanya matunda hata uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wafurahi pamoja. 37 Kwa maana katika hili neno hilo ni kweli, 'Mmoja hupanda na mwingine huvuna.' 38 Mimi naliwatuma kuvuna msichokitaabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao."
Samaria Yaamini
39 Na Wasamaria wengi wa mji ule wakamwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia akisema, "Aliniambia mambo yote niliyoyatenda." 40 Basi wale Wasamaria walipomjia, wakamsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. 41 Nao wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. 42 Wakamwambia yule mwanamke, "Sasa tunaamini, si kwa sababu ya maneno yako tu—kwa maana sisi wenyewe tumesikia, nasi twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu."
Kurudi Galilaya
43 Hata baada ya zile siku mbili aliondoka huko kwenda Galilaya. 44 (Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hana heshima katika nchi yake mwenyewe.) 45 Basi alipofika Galilaya, Wagalilaya wakamkaribisha, kwa kuwa wameyaona yote aliyoyafanya huko Yerusalemu kwenye sikukuu—maana wao nao walikuwa wamekwenda kwenye sikukuu. 46 Basi akaja tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe alikuwa hawezi huko Kapernaumu. 47 Huyu aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, akamwendea, akamsihi ashuke amponye mwanawe, kwa maana alikuwa karibu na kufa.
48 Basi Yesu akamwambia, "Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kamwe."
49 Yule diwani akamwambia, "Bwana, shuka kabla mwanangu hajafa."
50 Yesu akamwambia, "Enenda; mwanao yu hai." Yule mtu akaliamini lile neno Yesu alilomwambia, akaenda zake.
51 Hata alipokuwa akishuka, watumishi wake wakamlaki, wakamwambia ya kwamba mtoto wake yu hai. 52 Basi akawauliza saa aliyoanza kupata nafuu, wakamwambia, "Jana saa saba homa ilimwacha."
53 Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile Yesu aliyomwambia, "Mwanao yu hai." Akaamini yeye na nyumba yake yote.
54 Hii ndiyo ilikuwa ishara ya pili aliyoifanya Yesu alipokuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya.