Harusi huko Kana
2 1 Siku ya tatu, palikuwa na harusi huko Kana ya Galilaya; naye mama yake Yesu alikuwako. 2 Yesu naye pamoja na wanafunzi wake walikuwa wamealikwa arusini. 3 Divai ilipokwisha, mama yake Yesu akamwambia, "Hawana divai."
4 Yesu akamjibu, "Mama, kwa nini unaniingiza katika jambo hili? Saa yangu bado haijawadia."
5 Mama yake akawaambia watumishi, "Lolote atakalowaambia, lifanyeni."
6 Palikuwa na mitungi sita ya mawe iliyowekwa hapo kwa ajili ya utakaso wa Kiyahudi, kila mmoja ukichukua galoni ishirini hadi thelathini. a a v6 Kila mtungi ulichukua kama galoni 20 hadi 30 (lita 75 hadi 115) — hivi vilikuwa vyombo vikubwa.
7 Yesu akawaambia, "Jazeni mitungi maji," nao wakaijaza hata juu. 8 Akawaambia, "Sasa tekeni, mkampelekee mkuu wa karamu." Nao wakapeleka.
9 Mkuu wa karamu akayaonja yale maji yaliyokuwa yamekuwa divai, wala hakujua yalikotoka—ingawa watumishi walioyateka walijua. Basi akamwita bwana harusi kando 10 akamwambia, "Kila mtu huanza kuandaa divai iliyo nzuri, na ile duni baada ya wageni kulewa. Bali wewe umeiweka divai iliyo nzuri hata sasa." 11 Yesu alifanya ishara hii ya kwanza huko Kana ya Galilaya. Akaudhihirisha utukufu wake, na wanafunzi wake wakamwamini.
12 Baada ya hayo akashuka mpaka Kapernaumu, yeye na mama yake, na ndugu zake, na wanafunzi wake, wakakaa huko siku chache.
13 Pasaka ya Wayahudi ilipokuwa karibu, Yesu akapanda kwenda Yerusalemu.
Kusafisha Nyua za Hekalu
14 Ndani ya hekalu akawakuta wauzao ng'ombe, na kondoo, na njiwa, na wabadilishao fedha wameketi hapo. 15 Akafanya mjeledi wa kamba, akawafukuza wote katika nyua za hekalu, kondoo na ng'ombe pia, akaimwaga fedha za wabadilishaji, na kuzipindua meza zao.
16 Akawaambia wale wauzao njiwa, "Yaondoeni haya hapa! Msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa soko."
17 Wanafunzi wake wakakumbuka ya kuwa imeandikwa: "Wivu wa nyumba yako utanila."
18 Basi Wayahudi wakauliza, "Ni ishara gani utakayotuonyesha kwa kufanya mambo haya?"
19 Yesu akawajibu, "Livunjeni hekalu hili, nami katika siku tatu nitalisimamisha."
20 Wakajibu, "Hekalu hili lilijengwa kwa muda wa miaka arobaini na sita, nawe utalisimamisha katika siku tatu?" 21 Lakini yeye alikuwa akinena juu ya hekalu la mwili wake. 22 Basi alipofufuka katika wafu, wanafunzi wake wakakumbuka ya kwamba alikuwa amesema haya, wakaiamini Maandiko na neno lile alilolinena Yesu.
23 Alipokuwa Yerusalemu wakati wa Pasaka, watu wengi waliziona ishara alizozifanya, wakaliamini jina lake.
24 Lakini Yesu hakujitia kwao, kwa sababu yeye aliwajua watu wote. 25 Wala hakuhitaji mtu ye yote amshuhudie juu ya mwanadamu, kwa maana yeye alijua yaliyomo ndani ya kila mtu.