Nzi Waliokufa Katika Mafuta
Misemo juu ya jinsi kitu kidogo kinavyoweza kuharibu kingi: nzi waliokufa katika marashi, watumwa juu ya farasi na wakuu wakitembea kwa miguu, mpumbavu ajiangamizaye kwa maneno yake. Utulivu huituliza hasira ya mtawala; paa linaloinama na neno la uzembe chumbani cha kulala, vyote huanza vidogo.
10 1Nzi waliokufa huyafanya mafuta ya mtengeneza-marashi kunuka na kuchacha; vivyo hivyo upumbavu kidogo huzidi hekima na heshima. 2Moyo wa mwenye hekima huelekea upande wake wa kuume, bali moyo wa mpumbavu upande wake wa kushoto. 3Hata mpumbavu anapotembea njiani, hana akili, naye humwonyesha kila mtu kwamba yeye ni mpumbavu. 4Hasira ya mtawala ikikuwakia, usiache nafasi yako, kwa maana utulivu hutuliza makosa makuu.
5Kuna uovu niliouona chini ya jua, aina ile ya kosa litokalo kwa mtawala: 6upumbavu huwekwa katika mahali pengi pa juu, huku matajiri wakikaa katika nafasi za chini. 7Nimewaona watumwa wakiwa juu ya farasi, na wakuu wakitembea kwa miguu kama watumwa. 8Achimbaye shimo aweza kutumbukia ndani yake, naye abomoaye ukuta aweza kuumwa na nyoka. 9Achongaye mawe aweza kuumizwa nayo, naye apasuaye magogo aweza kupatwa na hatari kwa hayo. 10Ikiwa shoka ni butu wala makali yake hayajanolewa, ni lazima kutumia nguvu zaidi; lakini hekima huleta mafanikio.
11Ikiwa nyoka humwuma kabla hajalogwa, mlozi hapati faida yoyote. 12Maneno ya mtu mwenye hekima humletea kibali, bali midomo ya mpumbavu humwangamiza. 13Mwanzo wa maneno yake ni upumbavu, na mwisho wa mazungumzo yake ni wazimu mbaya. 14Lakini mpumbavu huzidi kuongea. Hakuna ajuaye linalokuja, naye ni nani awezaye kumwambia mtu yatakayotokea baada yake?
15Wapumbavu hujichosha kwa kazi zao, kwa maana hawaijui hata njia ya kwenda mjini. 16Ole wako, ee nchi, mfalme wako awapo mtoto na wakuu wako wafanyapo karamu asubuhi. 17Heri wewe, ee nchi, mfalme wako awapo mwana wa waungwana na wakuu wako wafanyapo karamu kwa wakati ufaao—kwa ajili ya nguvu, wala si kwa ulevi. 18Kwa sababu ya uvivu paa la nyumba huinama, na kwa sababu ya mikono legevu nyumba huvuja. 19Mkate hufanywa kwa ajili ya kicheko, na mvinyo huufurahisha uhai, na fedha hujibu mambo yote. 20Usimlaani mfalme hata katika mawazo yako, wala usiwalaani matajiri hata katika chumba chako cha kulala, kwa maana ndege wa angani aweza kuyachukua maneno yako, na kiumbe chenye mabawa chaweza kuripoti usemayo.