Kwa Sardi
Barua nyingine tatu. Sardi ina jina la kuwa hai nayo imekufa, matendo yake hayajakamilika mbele za Baba yake. Filadelfia ina nguvu kidogo lakini imelishika neno lake, kwa hiyo mlango uliofunguliwa ambao hakuna awezaye kuufunga. Laodikia inajiita tajiri nayo i uchi. Yeye anasimama akibisha, akingoja.
3 1"Kwa malaika wa kanisa lililoko Sardi andika: Yeye ashikaye zile Roho saba za Baba yetu na zile nyota saba asema hivi: Nayajua matendo yako. Una jina la kuwa hai, lakini u mfu.
2"Amka! Yaimarishe yaliyosalia yaliyo karibu kufa, kwa maana sikuyaona matendo yako yamekamilika mbele za Baba yangu. 3Basi kumbuka jinsi ulivyopokea na kusikia; yashike, na utubu. Usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutajua ni saa ipi nitakayokujia. 4Lakini una watu wachache katika Sardi ambao hawakuyachafua mavazi yao; nao watatembea pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa maana wanastahili. 5Yeye ashindaye atavikwa mavazi meupe kama wao, wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima. Nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu na mbele za malaika zake. 6Yeye aliye na sikio, na asikie yale Roho Mtakatifu ayaambiayo makanisa.
Kwa Filadelfia
7"Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika: Yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, ashikaye ufunguo wa Daudi, yeye afunguaye wala hakuna afungaye, afungaye wala hakuna afunguaye, asema hivi:
8"Nayajua matendo yako. Tazama, nimeweka mbele yako mlango uliofunguliwa ambao hakuna awezaye kuufunga, kwa sababu una nguvu kidogo, lakini umelishika neno langu wala hukulikana jina langu. 9Nitawatoa baadhi ya sinagogi la Shetani—wale wajiitao Wayahudi nao si Wayahudi, bali wanadanganya—nitawafanya waje wakusujudie miguuni pako, nao watajua ya kuwa nimekupenda. 10Kwa kuwa umelishika neno langu la saburi, mimi nami nitakulinda katika saa ya kujaribiwa itakayokuja juu ya ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi. 11Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, ili mtu asiitwae taji yako. 12Yeye ashindaye nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Baba yangu, wala hatatoka humo tena kamwe. Nami nitaandika juu yake jina la Baba yangu, na jina la mji wa Baba yangu, huo Yerusalemu mpya ushukao kutoka mbinguni kwa Baba yangu, na jina langu jipya. a a v12 Yesu anaposema juu ya Mungu hapa, anamtaja Baba — yeye aliyemtuma, ambaye anajenga hekalu lake, ambaye mji wake hushuka kutoka mbinguni. 13Yeye aliye na sikio, na asikie yale Roho Mtakatifu ayaambiayo makanisa.
Kwa Laodikia
14"Kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia andika: Yeye aliye Amina asema hivi, shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Baba yetu. b b v14 Yesu ndiye chanzo ambaye kwa yeye Baba yetu aliviumba vitu vyote — si kitu cha kwanza kuumbwa, bali ndiye ambaye kwa yeye viumbe vyote vilipata kuwako (Yohana 1:3; Wakolosai 1:16).
15"Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto. Laiti ungekuwa baridi au moto! 16Basi, kwa kuwa u vuguvugu, wala hu moto wala baridi, nakaribia kukutapika utoke kinywani mwangu. 17Kwa kuwa unasema, 'Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sihitaji kitu chochote,' nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, wa kuhurumiwa, maskini, kipofu, na uchi. 18Nakushauri: ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri; na mavazi meupe uyavae, aibu ya uchi wako isionekane; na dawa ya kupaka macho yako, upate kuona. 19Wale niwapendao mimi nawakemea na kuwarudi. Basi uwe na bidii, ukatubu. 20Tazama! Nasimama mlangoni, nabisha. Mtu akiisikia sauti yangu na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami. 21Yeye ashindaye nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nami nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi. 22Yeye aliye na sikio, na asikie yale Roho Mtakatifu ayaambiayo makanisa."