Kimbilio la Maisha Yote
71 1 Kwako, Baba yangu, ninakimbilia; nisiaibike kamwe. 2 Kwa haki yako unikomboe na uniponye; unisikilize na uniokoe. 3 Uwe mwamba wangu wa kimbilio, ambao naweza siku zote kuujia; umetoa amri ya kuniokoa, kwa maana wewe ndiwe mwamba wangu na ngome yangu. 4 Baba yangu, uniponye kutoka mkononi mwa mwovu, kutoka makuchani mwa mtu dhalimu na katili.
5 Kwa maana wewe ndiwe tumaini langu, Baba Mwenyezi, tegemeo langu tangu ujana wangu. 6 Nimekutegemea tangu kuzaliwa; wewe ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu. Ninakusifu siku zote. 7 Nimekuwa ajabu kwa wengi, lakini wewe ndiwe kimbilio langu imara. 8 Kinywa changu kimejaa sifa zako, na utukufu wako mchana kutwa.
9 Usinitupe wakati wa uzee wangu; nguvu zangu zikiisha, usiniache. 10 Kwa maana adui zangu wananena juu yangu; wanaovizia kuutwaa uhai wangu wanafanya shauri pamoja. 11 Wanasema, "Mungu amemwacha; mfuatilieni na kumkamata, kwa maana hakuna wa kumwokoa."
12 Baba yangu, usiwe mbali nami; Baba yangu, fanya haraka kunisaidia! 13 Washtaki wangu na waaibishwe na kuangamizwa; wanaotafuta kunidhuru na wafunikwe kwa dharau na fedheha.
14 Bali mimi nitatumaini daima, na nitakusifu zaidi na zaidi. 15 Kinywa changu kitasimulia haki yako, wokovu wako mchana kutwa, ijapokuwa sijui kipimo chake kamili. 16 Nitakuja nikitangaza matendo makuu ya Baba Mwenyezi; nitatangaza haki yako, yako peke yako.
17 Baba yangu, umenifundisha tangu ujana wangu, na hata leo natangaza matendo yako ya ajabu. 18 Hivyo hata nikiwa mzee na mwenye mvi, Baba yangu, usiniache, hata nitakapotangaza uweza wako kwa kizazi kingine, nguvu zako kwa wote watakaokuja.
19 Haki yako, Baba yangu, yafika mbingu za juu. Wewe uliyetenda mambo makuu, Baba yangu, ni nani aliye kama wewe? 20 Wewe uliyenionyesha taabu nyingi na misiba utanihuisha tena; kutoka vilindi vya nchi utanipandisha tena. 21 Utaongeza heshima yangu na kunifariji tena.
22 Nami nitakusifu kwa kinubi kwa uaminifu wako, Baba yangu; nitakuimbia sifa kwa zeze, Mtakatifu wa Israeli — Baba yangu. 23 Midomo yangu itapaza sauti kwa furaha nikuimbiapo sifa kwako, na nafsi yangu pia, uliyoikomboa. 24 Nao ulimi wangu utasimulia haki yako mchana kutwa, kwa maana waliotafuta kunidhuru wameaibishwa na kufedheheshwa.