Zaburi ya Daudi, ya kukumbusha.
38 1 Ee Baba wangu, usinikemee katika hasira yako, wala usiniadhibu katika ghadhabu yako. 2 Kwa maana mishale yako imenizama ndani sana, na mkono wako umenishukia kwa nguvu. 3 Hakuna afya mwilini mwangu kwa sababu ya hasira yako; hakuna uzima katika mifupa yangu kwa sababu ya dhambi yangu.
4 Kwa maana maovu yangu yamepanda juu ya kichwa changu; kama mzigo mzito, ni mzito kunizidi. 5 Vidonda vyangu vinanuka na kutunga usaha kwa sababu ya upumbavu wangu. 6 Nimeinama na kusujudu chini sana; mchana kutwa naenda nikiomboleza. 7 Kwa maana viuno vyangu vimejaa moto, wala hakuna uzima katika mwili wangu.
8 Nimekufa ganzi na kupondwa kabisa; naugua kwa sababu ya machafuko ya moyo wangu. 9 Ee Baba wangu Mwenye Enzi, shauku yangu yote iko mbele zako, wala kuugua kwangu hakukufichwa kwako. 10 Moyo wangu unadunda, nguvu zangu zinaniishia ; hata nuru ya macho yangu imeniondoka. 11 Rafiki zangu na wenzangu wanajitenga na mateso yangu, na jamaa zangu wa karibu wanasimama mbali.
12 Wale wanaoutafuta uhai wangu wanategesha mitego yao; wale wanaonitakia mabaya wananena maangamizi na kupanga hila mchana kutwa. 13 Lakini mimi ni kama kiziwi asiyesikia, kama bubu asiyeweza kusema wala hafumbui kinywa chake. 14 Nimekuwa kama mtu asiyesikia, ambaye hana jibu kinywani mwake. 15 Lakini nakungoja wewe, Baba wangu; ni wewe utakayejibu, Ee Baba wangu Mwenye Enzi.
16 Kwa maana nilisema, "Wasije kamwe wakanifurahia mimi—wale wanaojigamba juu yangu mguu wangu unapoteleza." 17 Kwa maana niko tayari kuanguka, na maumivu yangu yako mbele yangu daima. 18 Naungama uovu wangu; nasumbuka kwa sababu ya dhambi yangu. 19 Lakini adui zangu wana nguvu na wamejaa uhai, na wengi ni wale wanaonichukia bila sababu.
20 Wale wanaonilipa mabaya kwa mema wananishtaki kwa sababu nafuatia lililo jema. 21 Usiniache, Baba wangu; usisimame mbali nami, Baba wangu. 22 Fanya haraka kunisaidia , Ee Baba wangu Mwenye Enzi, wokovu wangu.