Unihukumie Haki, Baba
Zaburi ya Daudi.
26 1 Unihukumie haki, Baba yangu, kwa maana nimekwenda katika ukamilifu wangu, nami nimemtumaini Baba yangu bila kusita.
2 Unichunguze, Baba yangu, unijaribu; usafishe moyo wangu na akili yangu. 3 Kwa maana upendo wako wa agano u mbele ya macho yangu, nami naishi kwa uaminifu wako.
4 Sikai pamoja na watu wadanganyifu, wala sishirikiani na wanafiki. 5 Nachukia kusanyiko la watenda mabaya, wala sitaketi pamoja na waovu. 6 Ninanawa mikono yangu katika kutokuwa na hatia, nami nazunguka madhabahu yako, Baba yangu, 7 nikitangaza shukrani zangu kwa sauti, na kuhadithia matendo yako yote ya ajabu.
8 Baba yangu, naipenda nyumba unamokaa, mahali utukufu wako unapokaa.
9 Usiiondoe nafsi yangu pamoja na wenye dhambi, wala uhai wangu pamoja na watu wenye jeuri, 10 ambao mikononi mwao mna hila za uovu, na mikono yao ya kuume imejaa rushwa. 11 Bali mimi, naishi kwa ukamilifu; unikomboe na unifadhili.
12 Nasimama mahali penye usawa; katika kusanyiko kuu nitambariki Baba yangu.