Unilinde Dhidi ya Wenye Jeuri
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
140 1 Uniokoe, Baba yangu, na watu waovu; uniweke salama na wenye jeuri, 2 wanaopanga uovu mioyoni mwao na kuchochea vita mchana kutwa. 3 Wananoa ndimi zao kama nyoka; sumu ya fira i chini ya midomo yao. Sela
4 Unilinde, Baba yangu, na mikono ya waovu; uniweke salama na wenye jeuri, wanaopanga kunikwaza. 5 Wenye kiburi wamenifichia mtego; wametandaza kamba za wavu; kando ya njia wameniwekea tanzi. Sela
6 Nilimwambia Baba yangu, "Wewe ndiwe Baba yangu." Sikia sauti ya maombi yangu ya rehema. 7 Ee Baba Mwenye Enzi, nguvu ya wokovu wangu, umeikinga kichwa changu siku ya vita. 8 Usiwape, Baba yangu, waovu matakwa yao; usiache shauri lao lifanikiwe, wasije wakajiinua. Sela
9 Nao vichwa vya wale wanaonizunguka, taabu ya midomo yao wenyewe na iwafunike. 10 Makaa ya moto na yawaangukie; na watupwe motoni, katika mashimo ya matope, wasiinuke tena kamwe. 11 Mchongezi asithibitike nchini; uovu na umwinde mtu mwenye jeuri, pigo baada ya pigo.
12 Najua ya kuwa Baba yetu ataitetea haki ya mtu aliyeonewa na kumhukumia haki mhitaji. 13 Hakika wenye haki watalishukuru jina lako; wanyofu watakaa mbele zako.