Lisifuni Jina Lake
135 1 Haleluya! Lisifuni jina la Baba yetu; msifuni, enyi watumishi wa Baba yetu, 2 ninyi mnaohudumu katika nyumba ya Baba yetu, katika nyua za nyumba ya Baba yetu.
3 Msifuni Baba yetu, kwa maana Baba yetu ni mwema; liimbieni jina lake sifa, kwa maana ni kupendeza. 4 Kwa maana Baba yetu amejichagulia Yakobo, Israeli kuwa milki yake ya thamani.
5 Kwa maana najua ya kuwa Baba yetu ni mkuu, na Baba yetu mwenye enzi yu juu ya miungu yote. 6 Yote yaliyompendeza Baba yetu, ameyafanya, mbinguni na duniani, katika bahari na vilindi vyake vyote. 7 Yeye hupandisha mawingu toka miisho ya dunia; hufanya umeme kwa ajili ya mvua, na kuutoa upepo katika ghala zake.
8 Aliwapiga wazaliwa wa kwanza wa Misri, wa wanadamu na wa wanyama. 9 Alipeleka ishara na maajabu kati yako, Misri, juu ya Farao na watumishi wake wote. 10 Aliwapiga mataifa mengi, na kuwaua wafalme wenye nguvu— 11 Sihoni mfalme wa Waamori, na Ogu mfalme wa Bashani, na falme zote za Kanaani— 12 naye akaitoa nchi yao kuwa urithi, urithi kwa Israeli watu wake.
13 Jina lako, Baba yetu, ladumu milele; kumbukumbu lako, Baba yetu, kwa vizazi vyote. 14 Kwa maana Baba yetu atawatetea watu wake, na kuwahurumia watumishi wake.
15 Sanamu za mataifa ni fedha na dhahabu, kazi ya mikono ya wanadamu. 16 Zina vinywa, lakini haziwezi kunena; zina macho, lakini haziwezi kuona; 17 zina masikio, lakini haziwezi kusikia, wala hamna pumzi vinywani mwazo. 18 Wale wazitengenezao watakuwa kama hizo, na kila mtu anayezitumainia.
19 Enyi nyumba ya Israeli, mhimidini Baba yetu; enyi nyumba ya Haruni, mhimidini Baba yetu; 20 Enyi nyumba ya Lawi, mhimidini Baba yetu; ninyi mnaomcha Baba yetu, mhimidini Baba yetu. 21 Ahimidiwe Baba yetu toka Sayuni, yeye akaaye Yerusalemu. Haleluya!