Utukufu ni Wako
115 1 Si kwetu sisi, Baba yetu, si kwetu sisi, bali kwa jina lako uutukuze, kwa sababu ya upendo wako wa agano na uaminifu wako.
2 Mbona mataifa waseme, "Yuko wapi sasa Mungu wao?" 3 Baba yetu yuko mbinguni; hufanya lolote apendalo. 4 Sanamu zao ni fedha na dhahabu, kazi ya mikono ya wanadamu. 5 Zina vinywa, lakini haziwezi kusema; zina macho, lakini haziwezi kuona; 6 zina masikio, lakini haziwezi kusikia; zina pua, lakini haziwezi kunusa; 7 zina mikono, lakini haziwezi kupapasa; zina miguu, lakini haziwezi kutembea; wala sauti haitoki kooni mwao. 8 Wale wazitengenezao huwa kama hizo, na kila mtu anayezitumaini pia.
9 Ee Israeli, mtumaini Baba yetu! Yeye ndiye msaada wao na ngao yao. 10 Enyi nyumba ya Haruni, mtumaini Baba yetu! Yeye ndiye msaada wao na ngao yao. 11 Enyi mnaomcha Baba yetu, mtumaini yeye! Yeye ndiye msaada wao na ngao yao.
12 Baba yetu ametukumbuka; atatubariki sisi. Ataibariki nyumba ya Israeli; ataibariki nyumba ya Haruni; 13 atawabariki wanaomcha Baba yetu, wadogo kwa wakubwa.
14 Baba yetu na awaongeze zaidi na zaidi, ninyi na watoto wenu. 15 Mbarikiwe na Baba yetu, aliyeziumba mbingu na nchi.
16 Mbingu ni mbingu za Baba yetu, bali nchi amewapa wanadamu. 17 Wafu hawamsifu Baba yetu, wala wote washukao kwenye kimya. 18 Bali sisi tutambariki Baba yetu tangu sasa na hata milele. Haleluya!