Zaburi ya Daudi.
101 1 Juu ya upendo wa agano na haki nitaimba; kwako, Baba yangu, nitapiga muziki. 2 Nitakuwa mwangalifu kuifuata njia isiyo na lawama. Utakuja kwangu lini? Nitakwenda kwa unyofu wa moyo ndani ya nyumba yangu. 3 Sitaweka kitu kisichofaa mbele ya macho yangu. Nachukia kazi ya wale wanaokengeuka; haitanishika. 4 Moyo wa ukaidi utaondoka kwangu; sitajua neno lolote la uovu. 5 Yeyote kwa siri anayemsingizia jirani yake, huyo nitamnyamazisha; mwenye macho ya kiburi na moyo wa majivuno sitamvumilia. 6 Macho yangu yako kwa waaminifu wa nchi, ili wakae pamoja nami; yeye aendaye katika njia kamilifu atanitumikia. 7 Hakuna atendaye hila atakayekaa ndani ya nyumba yangu; hakuna asemaye uongo atakayesimama imara mbele ya macho yangu. 8 Kila asubuhi nitawanyamazisha waovu wote wa nchi, nikimkatilia mbali kila mtenda maovu kutoka mji wa Baba yetu.