Jasiri Kama Simba
Mamlaka na mali pamoja. Nchi inapoasi huwa na watawala wengi, mtawala mwovu ni kama dubu ashambuliaye, na watu hujificha waovu wainukapo. Kuficha dhambi hakufanikiwi, bali kuziungama hupata rehema, na kuharakisha kupata utajiri kunatajwa tena na tena kuwa ndiko kumwangamizako mtu.
28 1Waovu hukimbia ingawa hakuna anayewafuatia, bali wenye haki ni jasiri kama simba. 2Nchi inapoasi, huwa na watawala wengi, bali kwa mtu mwenye ufahamu na maarifa, hudumu imara. 3Maskini anayewaonea wanyonge ni kama mvua ya dhoruba isiyoacha chakula. 4Wale wanaoiacha sheria huwasifu waovu, bali wale wanaoishika sheria hupambana nao. 5Watu waovu hawaifahamu haki, bali wale wanaomtafuta Baba yetu huifahamu kikamilifu. 6Afadhali maskini anayeenenda kwa unyofu kuliko tajiri aliyepotoka katika njia zake. 7Yeye anayeishika sheria ni mwana mwenye ufahamu, bali rafiki wa walafi humwaibisha baba yake. 8Yeye anayeongeza mali yake kwa riba na faida ya udhalimu huikusanya kwa ajili ya yule mwenye ukarimu kwa maskini. 9Mtu akikataa kuisikiliza sheria, hata maombi yake ni chukizo. 10Yeye anayewapotosha wanyofu katika njia mbaya ataanguka katika shimo lake mwenyewe, bali wasio na hatia watarithi mema. 11Tajiri ana hekima machoni pake mwenyewe, bali maskini mwenye ufahamu humwona waziwazi. 12Wenye haki washindapo, kuna utukufu mkuu, bali waovu wainukapo, watu hujificha. 13Yeye afichaye dhambi zake hatafanikiwa, bali yeye anayeziungama na kuziacha atapata rehema. 14Amebarikiwa mtu anayedumu katika uchaji siku zote, bali yeye aufanyaye moyo wake mgumu ataanguka katika msiba. 15Kama simba angurumaye au dubu ashambuliaye ndivyo alivyo mtawala mwovu juu ya watu wanyonge. 16Mtawala asiye na ufahamu ni mdhalimu katili, bali yeye achukiaye faida ya udhalimu atazidisha siku zake. 17Mtu anayeelemewa na hatia ya kumwaga damu atakuwa mkimbizi hata kufa; mtu yeyote asimtegemeze. 18Yeye aenendaye kwa unyofu atalindwa salama, bali yeye aliyepotoka katika njia zake ataanguka ghafla. 19Yeye alimaye shamba lake atakuwa na mkate tele, bali yeye afuataye mambo matupu atakuwa na umaskini tele. 20Mtu mwaminifu atafurika baraka, bali yeye ahangaikaye kutajirika hataachwa bila adhabu. 21Kupendelea nyuso si vyema, lakini kwa kipande cha mkate mtu atatenda uovu. 22Mtu bahili ahangaika kupata mali naye hajui kuwa umaskini utampata. 23Yeye anayemkemea mtu hatimaye atapata upendeleo zaidi kuliko yule anayejipendekeza kwa ulimi wake. 24Yeye anayemwibia baba yake au mama yake na kusema, "Si dhambi," ni mwenzi wa yule aharibuye. 25Mtu mwenye tamaa huchochea ugomvi, bali yeye anayemtumaini Baba yetu atatajirishwa. 26Yeye anayeutumaini moyo wake mwenyewe ni mpumbavu, bali yeye aenendaye kwa hekima atalindwa salama. 27Yeye ampaye maskini hatapungukiwa na kitu, bali yeye anayewafumbia macho atapata laana nyingi. 28Waovu wainukapo, watu hujificha, bali waangamiapo, wenye haki hustawi.