Hezekia Mlangoni pa Mauti
Akiambiwa na Baba yetu kwamba hatapona, Hezekia anauelekeza uso wake ukutani na kulia. Anaongezewa miaka kumi na mitano, na kivuli cha jua kinarudi nyuma kuwa uthibitisho. Maombi yake aliyoyaandika hayaufichi uchungu wa kufa, nayo yanaishia kwa kujua kwamba walio hai ndio wamsifuo.
38 1Siku hizo Hezekia akaugua ugonjwa wa kufa. Nabii Isaya mwana wa Amozi akaja kwake na kumwambia, "Hivi ndivyo asemavyo Baba yetu: Tengeneza mambo ya nyumba yako, kwa maana utakufa; hutapona."
2Ndipo Hezekia akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Baba yetu, 3akasema, "Tafadhali, Baba yangu, kumbuka jinsi nilivyoenenda mbele zako kwa uaminifu na kwa moyo mkamilifu, nikafanya yaliyo mema machoni pako." Naye Hezekia akalia sana.
4Ndipo neno la Baba yetu likamjia Isaya:
5"Nenda ukamwambie Hezekia, 'Hivi ndivyo asemavyo Baba yetu, Baba wa baba yako Daudi: Nimeisikia sala yako, nami nimeyaona machozi yako. Tazama, nitaongeza miaka kumi na mitano katika maisha yako.' 6Nitakuokoa wewe na mji huu kutoka mkononi mwa mfalme wa Ashuru; nami nitaulinda mji huu.
7"Hii ndiyo ishara yako kutoka kwa Baba yetu kwamba atatimiza aliyoahidi: 8Tazama, nitakirudisha nyuma kivuli hatua kumi ambazo jua limeshuka juu ya ngazi ya Ahazi." Basi jua likarudi nyuma hatua kumi ambazo lilikuwa limeshuka.
9Maandiko ya Hezekia mfalme wa Yuda, baada ya kuugua kwake na kupona: 10Nikasema, "Katikati ya siku zangu ni lazima nipite katika malango ya kaburi; nimenyang'anywa miaka yangu iliyosalia." 11Nikasema, "Sitamwona Baba yetu mwenyewe katika nchi ya walio hai; sitawaangalia tena wanadamu, miongoni mwa wakaao katika ulimwengu huu upitao. 12Makao yangu yameng'olewa na kuchukuliwa mbali nami kama hema la mchungaji. Nimeyakunja maisha yangu kama mfumaji; yeye anikata kutoka katika kitanda cha kufumia; tangu mchana hata usiku unanikomesha. 13Nilingoja kwa utulivu hata asubuhi, lakini kama simba huvunja mifupa yangu yote; tangu mchana hata usiku unanikomesha. 14Kama mbayuwayu au korongo nalia; naugua kama hua. Macho yangu yamechoka kwa kutazama juu. Ee Baba Mwenye Enzi, nimeonewa; uwe dhamana yangu ya usalama!" 15Niseme nini? Ameniambia, naye mwenyewe ameyatenda. Nitakwenda taratibu miaka yangu yote kwa sababu ya uchungu wa nafsi yangu. 16Ee Baba Mwenye Enzi, kwa mambo kama hayo watu huishi, na katika hayo yote yamo maisha ya roho yangu. Basi unirudishe afya, na uniache niishi! 17Hakika ilikuwa kwa faida yangu mwenyewe kwamba nilipatwa na uchungu mkuu namna hii. Katika upendo wako umeyaokoa maisha yangu kutoka shimo la uharibifu, kwa maana umezitupa dhambi zangu zote nyuma ya mgongo wako. 18Kwa maana kaburi haliwezi kukusifu; mauti haiwezi kuimba sifa zako. Wale washukao shimoni hawawezi kuutumainia uaminifu wako. 19Walio hai, walio hai—hao ndio wanaokusifu, kama ninavyofanya mimi leo; baba huwajulisha watoto uaminifu wako. 20Baba yetu ataniokoa, nasi tutaziimba nyimbo zangu kwa vinanda vya nyuzi siku zote za maisha yetu, katika nyumba ya Baba yetu.
21Isaya alikuwa amesema, "Na watwae mkate wa tini, wauweke juu ya jipu, naye atapona." 22Hezekia alikuwa ameuliza, "Ni ishara gani kwamba nitapanda kwenda nyumba ya Baba yetu?"