Musa Anamwomba Baba wa Milele
Maombi ya Musa, mtu wa Baba yetu.
90 1 Baba Mwenye Enzi, wewe umekuwa makao yetu katika vizazi vyote. 2 Kabla milima haijazaliwa, wala kabla hujaiumba nchi na dunia, tangu milele hata milele wewe ndiwe Baba yetu.
3 Wawarudisha watu mavumbini, ukisema, "Rudini, enyi wanadamu."
4 Kwa maana miaka elfu machoni pako ni kama siku iliyokwisha kupita, kama kesha la usiku. 5 Wawagharikisha kama kwa mafuriko; wao ni kama ndoto, kama majani yachipukayo asubuhi— 6 asubuhi hustawi na kuchipuka; wakati wa jioni hunyauka na kukauka.
7 Kwa maana tumeangamizwa kwa hasira yako; kwa ghadhabu yako tumefadhaika. 8 Umeweka maovu yetu mbele zako, dhambi zetu za siri katika nuru ya uso wako. 9 Kwa maana siku zetu zote zapita chini ya ghadhabu yako; tunamaliza miaka yetu kama kuugua. 10 Tunaishi miaka sabini, au themanini ikiwa nguvu zetu zadumu; lakini haileti ila taabu na masikitiko—hupita upesi, nasi twaruka kwenda zetu. 11 Ni nani aijuaye nguvu ya hasira yako? Ghadhabu yako ni kubwa kama vile unavyostahili kuogopwa. 12 Utufundishe kuzihesabu siku zetu, tupate moyo wa hekima.
13 Urudi, Baba yetu! Hata lini? Uwahurumie watumishi wako. 14 Utushibishe asubuhi kwa upendo wako wa agano, tupate kuimba kwa furaha na kufurahi siku zetu zote. 15 Utufurahishe kwa kadiri ya siku ulizotutesa sisi, kwa kadiri ya miaka tuliyoyaona mabaya. 16 Watumishi wako na waione kazi yako, na watoto wao na wauone utukufu wako.
17 Neema ya Baba Mwenye Enzi na iwe juu yetu; uithibitishe kazi ya mikono yetu—naam, uithibitishe kazi ya mikono yetu.