Wimbo. Zaburi ya Asafu.
83 1 Ee Baba yetu, usinyamaze; usiwe kimya wala usitulie, Ee Baba yetu. 2 Maana tazama, adui zako wanafanya ghasia; wanaokuchukia wameinua vichwa vyao. 3 Juu ya watu wako wanafanya hila kwa siri; wanafanya shauri pamoja juu ya wale unaowathamini. 4 Wanasema, "Njoni, tuwaangamize wasiwe taifa; jina la Israeli lisikumbukwe tena." 5 Kwa nia moja wanafanya shauri; wamefanya agano juu yako— 6 mahema ya Edomu na Waishmaeli, Moabu na Wahagri, 7 Gebali na Amoni na Amaleki, Ufilisti pamoja na wenyeji wa Tiro. 8 Ashuru naye ameungana nao; wamekuwa mkono wa nguvu wa wana wa Loti. Sela
9 Uwatendee kama ulivyowatendea Midiani, kama Sisera na Yabini penye mto Kishoni, 10 walioangamizwa huko En-dori wakawa samadi ya nchi. 11 Wafanye wakuu wao kama Orebu na Zeebu, na maakida wao wote kama Zeba na Salmuna, 12 waliosema, "Na tujitwalie malisho ya Mungu." 13 Ee Baba yangu, uwafanye kama mavumbi yazungukayo, kama makapi mbele ya upepo. 14 Kama moto uteketezavyo msitu, kama mwali uwashavyo milima moto, 15 vivyo hivyo uwafuatie kwa tufani yako na kuwatia hofu kwa dhoruba yako. 16 Funika nyuso zao kwa aibu, ili walitafute jina lako, Ee Baba yetu. 17 Waaibike na kufadhaika milele; waangamie kwa fedheha, 18 ili wajue ya kuwa wewe peke yako, ambaye jina lako ni Baba yetu, ndiwe Uliye Juu Sana juu ya dunia yote.