Baba Yetu Ni Mwema
Zaburi ya Asafu.
73 1 Hakika Baba yetu ni mwema kwa Israeli, kwa wale walio safi wa moyo.
2 Bali mimi, miguu yangu ilikaribia kujikwaa; hatua zangu zilikaribia kuteleza. 3 Kwa maana niliwaonea wivu wenye kiburi nilipoona kufanikiwa kwa waovu. 4 Kwa maana hawana maumivu katika kufa kwao; miili yao ina afya na imenona. 5 Hawamo katika taabu kama watu wengine; hawapigwi kama wanadamu wengine. 6 Kwa hiyo kiburi ni mkufu wao; jeuri huwafunika kama vazi. 7 Macho yao yanatokeza kwa unene; mawazo ya mioyo yao hupita kiasi. 8 Hudhihaki na kunena kwa hila; kutoka juu hutishia udhalimu. 9 Huelekeza vinywa vyao juu mbinguni, na ulimi wao hupita duniani kwa majivuno. 10 Kwa hiyo watu wake huwageukia, na kunywa maji tele. 11 Nao husema, "Mungu ajuaje? Je, kuna maarifa kwake Aliye Juu?" 12 Tazama — hawa ndio waovu; siku zote wako raha, wanazidi kupata utajiri.
13 Hakika nimeutakasa moyo wangu bure na kunawa mikono yangu katika kutokuwa na hatia. 14 Kwa maana mchana kutwa nimepigwa na kukaripiwa kila asubuhi.
15 Kama ningesema, "Nitanena hivi," ningaliisaliti kizazi cha watoto wako. 16 Nilipojaribu kuelewa haya yote, ilikuwa kazi ya kutaabisha machoni pangu, 17 hata nilipoingia patakatifu pa Baba yetu; ndipo nilipoelewa mwisho wao. 18 Hakika unawaweka mahali penye utelezi; unawaangusha kwenye maangamizi. 19 Jinsi wanavyoangamizwa ghafula, wamefagiliwa mbali kabisa na vitisho! 20 Kama ndoto mtu aamkapo, Ee Baba Mwenye Enzi, utakapoinuka, utawadharau kama vivuli.
21 Moyo wangu ulipojaa uchungu nami nilipochomwa ndani, 22 Nilikuwa mpumbavu na sijui kitu; nilikuwa kama mnyama mbele yako. 23 Walakini mimi niko pamoja nawe daima; umenishika mkono wangu wa kuume. 24 Unaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipokea katika utukufu. 25 Nina nani mbinguni ila wewe? Wala hakuna duniani nitakachokitamani ila wewe. 26 Mwili wangu na moyo wangu vyaweza kulegea, lakini Baba yetu ndiye nguvu za moyo wangu na fungu langu milele.
27 Kwa maana wale walio mbali nawe wataangamia; unamwangamiza kila mtu asiye mwaminifu kwako. 28 Bali kwangu mimi, ni vyema kuwa karibu na Baba yetu; nimemfanya Baba Mwenye Enzi kimbilio langu, ili nipate kuyatangaza matendo yako yote.