Wimbo wa Kuwekwa Wakfu
Zaburi. Wimbo wa kuwekwa wakfu kwa nyumba. Ya Daudi.
30 1 Nitakutukuza, Baba yangu, kwa kuwa ulininyanyua, wala hukuwaacha adui zangu wanifurahie.
2 Baba yangu, nilikulilia unisaidie, nawe ukaniponya. 3 Baba yangu, uliipandisha nafsi yangu kutoka kaburini; ulinihifadhi hai, wala hukuniacha nishuke shimoni.
4 Mwimbieni Baba yetu, enyi watauwa wake, mkalishukuru jina lake takatifu. 5 Kwa maana hasira yake ni ya kitambo kidogo, bali kibali chake ni cha maisha yote; kilio chaweza kukaa usiku kucha, lakini furaha huja asubuhi.
6 Nilipokuwa salama, nilisema, "Sitatikisika kamwe." 7 Baba yangu, kwa kibali chako uliusimamisha mlima wangu imara; lakini ulipouficha uso wako, nikafadhaika.
8 Kwako, Baba yangu, naliita; kwa Baba Mwenye Enzi naliomba rehema: 9 "Kuna faida gani nikinyamazishwa, nikishuka shimoni? Je, mavumbi yatakusifu wewe? Yatatangaza uaminifu wako?" 10 Nisikie, Baba yangu, unifadhili; Baba yangu, uwe msaidizi wangu.
11 Uligeuza maombolezo yangu kuwa kucheza; ulinivua nguo zangu za maombolezo, ukanivika furaha, 12 ili moyo wangu ukuimbie sifa wala usinyamaze. Baba yangu, nitakushukuru milele.