Zaburi ya Daudi.
103 1 Ee nafsi yangu, umhimidi Baba yetu; na vyote vilivyo ndani yangu, vihimidi jina lake takatifu!
2 Ee nafsi yangu, umhimidi Baba yetu, wala usisahau fadhili zake zote— 3 akusamehaye maovu yako yote, akuponyaye magonjwa yako yote, 4 aukomboaye uhai wako na kaburi, akuvikaye taji ya upendo thabiti na huruma, 5 akushibishaye kwa mema maadamu unaishi, hata ujana wako ukafanywa upya kama tai.
6 Baba yetu hutenda haki na hukumu ya adili kwa wote wanaoonewa.
7 Alimjulisha Musa njia zake, matendo yake kwa wana wa Israeli. 8 Baba yetu ni mwenye huruma na neema, si mwepesi wa hasira, tena ni mwingi wa upendo thabiti. 9 Hatalaumu siku zote, wala hatashika hasira yake milele. 10 Hakututenda sawasawa na dhambi zetu, wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. 11 Kwa maana kama mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, ndivyo upendo wake thabiti ulivyo mkuu kwa wamchao; 12 Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoziweka dhambi zetu mbali nasi.
13 Kama vile moyo wa baba unavyowahurumia watoto wake, ndivyo moyo wa Baba yetu unavyowahurumia wamchao. 14 Kwa maana yeye anajua umbo letu; anakumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi. 15 Siku za mwanadamu ni kama majani; huchanua kama ua la porini shambani; 16 kwa maana upepo hupita juu yake, nalo hutoweka, wala mahali pake hapapalikumbuki tena. 17 Bali upendo thabiti wa Baba yetu ni tangu milele hata milele juu ya wale wamchao, na haki yake kwa watoto wa watoto, 18 kwa wale walishikao agano lake, na kukumbuka kuyatenda maagizo yake.
19 Baba yetu ameuweka kiti chake cha enzi mbinguni, na ufalme wake unatawala juu ya vyote.
20 Mhimidini Baba yetu, enyi malaika zake, enyi mashujaa mtendao neno lake, mkitii sauti ya neno lake! 21 Mhimidini Baba yetu, enyi majeshi yake yote, watumishi wake mtendao mapenzi yake! 22 Mhimidini Baba yetu, enyi kazi zake zote, katika mahali pote pa ufalme wake. Ee nafsi yangu, umhimidi Baba yetu!