Baba yetu Huchunguza Mioyo
17 1Afadhali kipande kikavu cha mkate kinacholiwa kwa amani kuliko nyumba iliyojaa karamu pamoja na ugomvi. 2Mtumishi mwenye busara atamtawala mwana aaibishaye, naye atagawana urithi pamoja na ndugu. 3Kalibu ni kwa ajili ya fedha na tanuru kwa ajili ya dhahabu, bali Baba yetu huichunguza mioyo. 4Mtenda maovu huyasikiliza midomo miovu; mwongo huusikiliza ulimi uharibuo. 5Amdhihakiye maskini humtukana Muumba wake; afurahiaye msiba hataacha kuadhibiwa. 6Wajukuu ni taji ya wazee, na utukufu wa watoto ni wazazi wao. 7Maneno mazuri hayampasi mpumbavu—sembuse midomo ya uongo kwa mtu mwenye heshima. 8Rushwa huonekana kama hirizi ya uganga machoni pa yule aitoaye; kila aendako, hudhani atafanikiwa. 9Afunikaye kosa hutafuta upendo, bali azidiye kulikumbusha hutenganisha rafiki wa karibu. 10Karipio huingia ndani zaidi kwa mtu mwenye ufahamu kuliko mapigo mia moja kwa mpumbavu. 11Mtu mwasi hutafuta mabaya tu, naye mjumbe katili atatumwa dhidi yake. 12Afadhali kukutana na dubu aliyenyang'anywa watoto wake kuliko mpumbavu katika upumbavu wake. 13Mtu akirudisha ovu badala ya jema, ovu halitaondoka nyumbani mwake kamwe. 14Kuanzisha ugomvi ni kama kupasua tuta la maji, basi acha mateto kabla hayajafurika. 15Amhesabiaye haki mtu mwovu na amhukumuye mtu mwenye haki—wote wawili ni chukizo kwa Baba yetu. 16Kwa nini mpumbavu awe na fedha mkononi ili kununua hekima, wakati hana moyo wa kujifunza? 17Rafiki hupenda wakati wote, na ndugu huzaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu. 18Mtu asiye na akili hupeana mkono kwa ahadi na kuweka dhamana kwa ajili ya jirani yake. 19Apendaye kutenda mabaya hupenda ugomvi; ajengaye lango lake juu hukaribisha uharibifu. 20Moyo uliopotoka haupati jema lolote, na ulimi wenye hila huanguka katika taabu. 21Amzaaye mpumbavu hujiletea huzuni; baba wa mpumbavu asiyemcha Mungu hana furaha. 22Moyo wenye furaha ni dawa nzuri, bali roho iliyopondeka huikausha mifupa. 23Mtu mwovu huchukua rushwa kwa siri ili kupotosha njia za haki. 24Mtu mwenye ufahamu huitunza hekima mbele ya macho yake, bali macho ya mpumbavu hutangatanga hata miisho ya dunia. 25Mwana mpumbavu ni huzuni kwa babaye na uchungu kwa mama aliyemzaa. 26Kumwadhibu mwenye haki si vyema, wala kumpiga mtu mwenye heshima kwa unyofu wake. 27Azuiaye maneno yake ana maarifa, na mtu mwenye roho tulivu ni mtu mwenye ufahamu. 28Hata mpumbavu akinyamaza huhesabiwa kuwa mwenye hekima; afumbapo midomo yake, huonekana mwenye ufahamu.