Tumaini Lililoahirishwa, Shauku Iliyotimizwa
13 1Mwana mwenye hekima husikiliza mafundisho ya baba yake, bali mwenye dharau hasikilizi karipio. 2Kutokana na tunda la kinywa chake mtu hufurahia mema, bali shauku ya wadanganyifu ni jeuri. 3Yeye alindaye kinywa chake huhifadhi uhai wake, bali afunuaye midomo yake sana huangamia. 4Mtu mvivu hutamani, wala hapati kitu, bali shauku ya mwenye bidii hushibishwa kwa wingi. 5Mwenye haki huchukia uongo, bali mwovu huleta aibu na fedheha. 6Haki humlinda yeye ambaye njia yake haina lawama, bali uovu humwangusha mwenye dhambi. 7Mtu mmoja hujifanya tajiri, hali hana kitu; mwingine hujifanya maskini, hali ana mali nyingi. 8Mali ya mtu yaweza kukomboa uhai wake, bali maskini hasikii kitisho. 9Nuru ya mwenye haki huangaza kwa furaha, bali taa ya mwovu itazimwa. 10Kiburi hazai kitu ila ugomvi, bali hekima hukaa na wale watafutao shauri. 11Mali ipatikanayo kwa udanganyifu hupungua, bali yeye akusanyaye kidogo kidogo huiongeza. 12Tumaini lililoahirishwa huugumza moyo, bali shauku iliyotimizwa ni mti wa uzima. 13Yeye alidharauye neno hujiletea maangamizi, bali yeye aiheshimuye amri atapewa thawabu. 14Fundisho la mwenye hekima ni chemchemi ya uzima, limgeuzayo mtu mbali na mitego ya mauti. 15Akili njema huvuta kibali, bali njia ya wadanganyifu ni maangamizi yao. 16Kila mtu mwenye busara hutenda kwa maarifa, bali mpumbavu huonyesha upumbavu wake. 17Mjumbe mwovu huanguka katika taabu, bali mjumbe mwaminifu huleta uponyaji. 18Umaskini na aibu humpata yeye asiyejali adabu, bali yeye asikiaye karipio huheshimiwa. 19Shauku iliyotimizwa ni tamu nafsini, bali kujiepusha na uovu ni chukizo kwa wapumbavu. 20Yeye atembeaye na wenye hekima huwa na hekima, bali rafiki wa wapumbavu hupatwa na madhara. 21Msiba huwafuatia wenye dhambi, bali mema huwalipa wenye haki. 22Mtu mwema huwaachia wajukuu wake urithi, bali mali ya mwenye dhambi huwekwa akiba kwa ajili ya wenye haki. 23Shamba la maskini lisilolimwa laweza kutoa chakula tele, bali huchukuliwa mbali kwa kukosa haki. 24Yeye azuiaye fimbo humchukia mwanawe, bali yeye ampendaye humwadibu kwa bidii. 25Mwenye haki hula hata ashibe moyoni mwake, bali tumbo la mwovu hukaa na njaa.