Mithali za Sulemani Zaanza
10 1Mithali za Sulemani: Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye, bali mwana mpumbavu humhuzunisha mamaye. 2Hazina zilizopatikana kwa uovu hazifai kitu, bali haki huokoa na mauti. 3Baba yetu hatamwacha mwenye haki apate njaa, bali hupinga tamaa ya waovu. 4Mikono ya uvivu hukufanya maskini, bali mikono yenye bidii huleta utajiri. 5Yeye akusanyaye wakati wa kiangazi ni mwana mwenye busara, bali yeye alalaye wakati wa mavuno ni mwana aletaye aibu. 6Baraka hukaa juu ya kichwa cha mwenye haki, bali kinywa cha waovu hufunika jeuri. 7Kumbukumbu ya mwenye haki ni baraka, bali jina la waovu litaoza. 8Moyo wenye hekima hupokea maagizo, bali mpumbavu apayukaye huangamia. 9Yeye aendaye kwa unyofu huenda salama, bali yeye azipotoshaye njia zake atagunduliwa. 10Yeye akonyezaye kwa jicho huleta taabu, na mpumbavu apayukaye huangamia. 11Kinywa cha mwenye haki ni chemchemi ya uzima, bali kinywa cha waovu hufunika jeuri. 12Chuki huchochea ugomvi, bali upendo hufunika makosa yote. 13Katika midomo ya mwenye ufahamu, hekima hupatikana, bali fimbo ni kwa mgongo wa asiye na akili. 14Wenye hekima huhifadhi maarifa, bali kinywa cha mpumbavu hukaribisha uharibifu. 15Mali ya tajiri ndicho mji wake wenye ngome; uharibifu wa maskini ni umaskini wao. 16Ujira wa mwenye haki huelekea uzimani; faida ya waovu huelekea dhambini. 17Yeye apokeaye adabu yumo katika njia ya uzima, bali yeye apuuzaye maonyo huwapotosha wengine. 18Yeye afichaye chuki ni mwongo, na yeye aenezaye masingizio ni mpumbavu. 19Palipo na maneno mengi, dhambi haikosekani; bali yeye auzuiaye ulimi wake ana hekima. 20Ulimi wa mwenye haki ni fedha iliyo bora; moyo wa waovu una thamani ndogo. 21Midomo ya mwenye haki hulisha wengi, bali wapumbavu hufa kwa kukosa akili. 22Baraka ya Baba yetu huleta utajiri, wala hachanganyi huzuni pamoja nayo. 23Kutenda uovu ni mchezo kwa mpumbavu, bali hekima ni furaha ya mtu mwenye ufahamu. 24Kile anachokiogopa mwovu kitampata, bali haja ya mwenye haki itatimizwa. 25Dhoruba ikiisha kupita, waovu hutoweka, bali wenye haki husimama imara milele. 26Kama siki kwa meno na moshi kwa macho, ndivyo alivyo mvivu kwa wale wamtumao. 27Kumcha Baba yetu huongeza siku za maisha, bali miaka ya waovu itafupishwa. 28Tumaini la mwenye haki huleta furaha, bali matarajio ya waovu yataangamia. 29Njia ya Baba yetu ni kimbilio kwa wanyofu, bali ni uharibifu kwa watendao mabaya. 30Mwenye haki hatatikiswa kamwe, bali waovu hawatakaa katika nchi. 31Kinywa cha mwenye haki hutoa hekima, bali ulimi wa upotovu utakatiliwa mbali. 32Midomo ya mwenye haki hujua yanayokubalika, bali kinywa cha waovu hujua yaliyo potovu tu.