Sadaka ya Hatia
6 1Baba yetu akanena na Musa:
2"Mtu ye yote akifanya dhambi, akiwa si mwaminifu kwa Baba yako, kwa kumdanganya jirani yake kuhusu amana, au rehani, au vitu vilivyoibwa, au kwa kumpunja, 3au kama akipata kitu kilichopotea na kudanganya kuhusu hicho, akiapa kwa uongo—jambo lo lote la namna hiyo ambalo kwalo mtu hufanya dhambi. 4Atakapofanya dhambi na kupatikana na hatia, ni lazima arudishe kile alichoiba, au alichonyakua kwa nguvu, au ile amana aliyokabidhiwa, au kile kilichopotea alichokipata, 5au cho chote alichoapia kwa uongo, ni lazima akilipe kikamilifu, aongeze juu yake sehemu ya tano, na akimpe mwenyewe siku ile atakapokiri hatia yake. 6Naye atamletea Baba yako sadaka yake ya hatia: kondoo dume asiye na dosari kutoka katika kundi, kwa kadiri ya thamani uliyoiweka, kuwa sadaka ya hatia, kwa kuhani. 7Kuhani atamfanyia upatanisho mbele za Baba yako, naye atasamehewa kwa lo lote alilotenda lililomfanya awe na hatia."
Sadaka ya Kuteketezwa
8Kisha Baba yetu akanena na Musa:
9"Waamuru Haruni na wanawe: Hii ndiyo sheria ya sadaka ya kuteketezwa. Itakaa juu ya moto wa madhabahu usiku kucha hata asubuhi, na moto wa madhabahu utaendelea kuwaka juu yake. 10Kuhani atavaa vazi lake la kitani, akiwa na nguo za ndani za kitani mwilini mwake, kisha atayaondoa yale majivu yaliyosalia baada ya moto kuiteketeza sadaka ya kuteketezwa juu ya madhabahu, na atayaweka kando ya madhabahu. 11Kisha atavua mavazi yake, avae mengine, na kuyachukua yale majivu nje ya kambi hata mahali safi. 12Moto wa madhabahu utaendelea kuwaka; haupasi kuzimika. Kila asubuhi kuhani ataongeza kuni juu yake, atapanga sadaka ya kuteketezwa juu yake, na kuteketeza mafuta ya sadaka za amani juu yake. 13Moto utaendelea kuwaka juu ya madhabahu daima; haupasi kuzimika.
Sadaka ya Nafaka
14"Hii ndiyo sheria ya sadaka ya nafaka: Wana wa Haruni watailete mbele za Baba yako, mbele ya madhabahu. 15Kuhani atatwaa konzi moja ya unga mzuri wa sadaka ya nafaka na mafuta yake, pamoja na uvumba wake wote, na kuiteketeza sehemu hii ya ukumbusho juu ya madhabahu kuwa harufu nzuri ya kumpendeza Baba yako. 16Haruni na wanawe watakula kilichosalia; ni lazima kiliwe bila chachu mahali patakatifu, kiliwe katika ua wa hema ya kukutania. 17Msikioke kwa chachu. Nimekitoa kuwa fungu lao katika sadaka zangu za kutolewa kwa moto, kama sadaka ya dhambi na sadaka ya hatia; ni kitakatifu sana. 18Kila mwanamume miongoni mwa wazao wa Haruni aweza kukila—ni fungu la milele katika vizazi vyenu kutoka katika sadaka za Baba yako zinazotolewa kwa moto. Kila kitakachozigusa kitakuwa kitakatifu."
19Baba yetu akamwambia Musa:
20"Hii ndiyo sadaka ya Haruni na wanawe watakayomtolea Baba yako siku ile atakapotiwa mafuta: kama lita moja ya unga mzuri kuwa sadaka ya nafaka ya daima, nusu yake asubuhi na nusu yake jioni. 21Utaiandaa kwa mafuta juu ya kaango, uilete ikiwa imekandwa vizuri, uitoe sadaka ya nafaka katika vipande vilivyovunjwa—harufu nzuri ya kumpendeza Baba yako. 22Kuhani atakayetiwa mafuta atakayeingia mahali pake miongoni mwa wanawe ataiandaa—ni amri ya milele mbele za Baba yako: ni lazima iteketezwe kabisa. 23Kila sadaka ya nafaka ya kuhani itateketezwa kabisa; haipasi kuliwa."
Sadaka ya Dhambi
24Tena Baba yetu akanena na Musa:
25"Waambie Haruni na wanawe: hii ndiyo sheria ya sadaka ya dhambi: itachinjwa mbele za Baba yako, mahali ile sadaka ya kuteketezwa ichinjwapo; ni takatifu sana. 26Kuhani anayeitoa kwa ajili ya dhambi ni lazima aile; italiwa mahali patakatifu, katika ua wa hema ya kukutania. 27Kila kitakachogusa nyama yake kitakuwa kitakatifu. Na damu yake ikinyunyizwa juu ya vazi, utapafua mahali paliponyunyizwa mahali patakatifu. 28Chungu cha udongo kilichotokosewa lazima kivunjwe; na kama kimetokosewa katika chungu cha shaba, ni lazima kisuguliwe na kusuuzwa kwa maji. 29Kila mwanamume miongoni mwa makuhani aweza kuila; ni takatifu sana. 30Hakuna sadaka ya dhambi ambayo damu yake huletwa ndani ya hema ya kukutania kufanya upatanisho katika Patakatifu itakayoliwa; ni lazima iteketezwe kwa moto."