Mkono wa Baba katika Ndoa ya Samsoni
14 1Samsoni akashuka mpaka Timna, akamwona huko mwanamke kijana, mmoja wa binti za Wafilisti. 2Akapanda na kuwaambia baba yake na mama yake, "Nimemwona mwanamke Mfilisti huko Timna; sasa nipatieni yeye awe mke wangu."
3Baba yake na mama yake wakamwambia, "Je, hakuna mwanamke miongoni mwa jamaa zako au katika watu wangu wote, hata ulazimike kutwaa mke kutoka kwa Wafilisti wasiotahiriwa?" Lakini Samsoni akamwambia baba yake, "Nipatie huyo; ndiye anayenipendeza machoni pangu."
4Baba yake na mama yake hawakujua kwamba jambo hili lilitoka kwa Baba yetu, aliyekuwa akitafuta sababu ya kuwashambulia Wafilisti, kwa maana wakati ule Wafilisti waliitawala Israeli.
5Basi Samsoni akashuka mpaka Timna pamoja na baba yake na mama yake. Walipofika kwenye mashamba ya mizabibu ya Timna, tazama, mwana-simba akamjia akinguruma. 6Roho wa Baba yetu akamjilia kwa nguvu, naye akampasua yule simba vipande viwili kwa mikono yake mitupu kama vile aichanavyo mwana-mbuzi, lakini hakuwaambia baba yake wala mama yake alichokifanya. 7Kisha akashuka, akazungumza na yule mwanamke, naye alimpendeza Samsoni machoni pake.
8Baadaye, aliporudi ili kumwoa, akageuka kando ili kuutazama mzoga wa yule simba. Na tazama, ndani yake mlikuwa na kundi la nyuki, na asali. 9Akaikwangua ile asali mikononi mwake, akala huku akitembea. Alipowafikia baba yake na mama yake, akawapa nao wakala. Lakini hakuwaambia kwamba alikuwa ameikwangua asali kutoka mzoga wa simba. 10Basi baba yake akashuka kwa yule mwanamke, naye Samsoni akafanya karamu huko, kama walivyokuwa wakifanya vijana. 11Watu walipomwona, wakaleta wenzake thelathini ili wawe pamoja naye.
12Samsoni akawaambia, "Ngoja niwategee kitendawili. Kama mtakiteguo ndani ya siku saba za karamu, nami nitawapa mavazi thelathini ya kitani na mavazi thelathini ya kubadilisha. 13Lakini kama hamtaweza kunijibu, ndipo ninyi mnipe mavazi thelathini ya kitani na mavazi thelathini ya kubadilisha." Wakamwambia, "Tega kitendawili chako; na tukisikie."
14Akawaambia, "Katika mlaji kilitoka kitu cha kuliwa; katika mwenye nguvu kilitoka kitu kitamu." Kwa muda wa siku tatu wakashindwa kukitegua kile kitendawili.
15Siku ya nne wakamwambia mke wa Samsoni, "Mbembeleze mumeo atueleze maana ya kile kitendawili, la sivyo tutakuteketeza wewe na nyumba ya baba yako kwa moto. Je, mmetualika hapa ili kutunyang'anya mali zetu?"
16Mke wa Samsoni akamlilia, akisema: "Wewe wanichukia tu; hunipendi. Umewategea watu wangu kitendawili, lakini hujaniambia mimi maana yake." Akamwambia, "Tazama, sijawaambia baba yangu wala mama yangu, nikuambie wewe?"
17Akamlilia siku zile saba za karamu yao, na siku ya saba akamwambia, kwa sababu alimshinikiza sana. Kisha akawaambia watu wake kile kitendawili. 18Siku ya saba, kabla jua halijazama, watu wa mji wakamwambia, "Kitu gani kilicho kitamu kuliko asali? Kitu gani kilicho na nguvu kuliko simba?" Samsoni akawajibu, "Kama hamkulima kwa ndama wangu wa ng'ombe, msingekitegua kamwe kitendawili changu."
19Ndipo Roho wa Baba yetu akamjilia kwa nguvu. Akashuka mpaka Ashkeloni, akawaua watu thelathini miongoni mwao, akatwaa mateka yao, akawapa mavazi yao wale walioutegua kitendawili. Naye akiwaka hasira, akapanda kwenda nyumbani kwa baba yake. 20Naye mke wa Samsoni akapewa kwa mwenzake, yule aliyekuwa mstari wa mbele katika arusi yake.