Baba Aahidi Mwana
13 1Wana wa Israeli wakafanya tena maovu machoni pa Baba yetu, naye akawatia mkononi mwa Wafilisti muda wa miaka arobaini.
2Palikuwa na mtu mmoja jina lake Manoa, wa Sora, wa jamaa ya Wadani, na mkewe alikuwa tasa, hakuzaa watoto.
3Malaika wa Baba yetu akamtokea yule mwanamke, akamwambia, "Tazama, wewe u tasa, huna mtoto, lakini utachukua mimba na kuzaa mwana. 4Basi sasa, jihadhari usinywe divai wala kileo, wala usile kitu chochote kilicho najisi, 5kwa maana utachukua mimba na kuzaa mwana. Wembe usipite kichwani pake, kwa maana mtoto huyo atakuwa mnadhiri wa Baba yetu tangu tumboni, naye ataanza kuwaokoa Israeli mkononi mwa Wafilisti."
6Yule mwanamke akaenda, akamwambia mumewe, "Mtu wa Mungu alinijia; sura yake ilikuwa kama sura ya malaika wa Baba yetu, ya kutisha sana. Sikumwuliza atokako, wala hakuniambia jina lake." 7Lakini aliniambia, 'Utachukua mimba na kuzaa mwana. Basi sasa usinywe divai wala kileo, wala usile kitu chochote kilicho najisi, kwa maana mtoto huyo atakuwa mnadhiri wa Baba yetu tangu tumboni hata siku ya kufa kwake.'"
8Ndipo Manoa akamsihi Baba yetu, akasema, "Ee Bwana wangu Baba, tafadhali yule mtu wa Mungu uliyemtuma na aje kwetu tena, atufundishe tumfanyie nini mtoto atakayezaliwa."
9Baba yetu akaisikia sauti ya Manoa; malaika wa Baba yetu akamjia tena yule mwanamke alipokuwa ameketi shambani, lakini Manoa mumewe hakuwa pamoja naye. 10Yule mwanamke akakimbia upesi, akamwambia mumewe, "Tazama, yule mtu aliyenijia siku ile amenitokea!"
11Manoa akaondoka, akamfuata mkewe, akamfikia yule mtu. Akamwuliza, "Je, wewe ndiwe yule mtu uliyesema na huyu mwanamke?" Akajibu, "Mimi ndiye."
12Manoa akasema, "Basi maneno yako yatakapotimia, ni nini kitakachotawala maisha na kazi ya mtoto huyo?"
13Malaika wa Baba yetu akamwambia Manoa, "Yule mwanamke na ajihadhari na yote niliyomwambia. 14Asile kitu chochote kitokacho katika mzabibu, wala asinywe divai au kileo, wala asile kitu chochote kilicho najisi. Na ashike yote niliyomwamuru."
15Manoa akamwambia malaika wa Baba yetu, "Tafadhali turuhusu tukuzuie, nasi tutakuandalia mwana-mbuzi."
16Malaika wa Baba yetu akamwambia Manoa, "Hata ukanizuia, sitakula chakula chako; lakini ukiandaa sadaka ya kuteketezwa, umtolee Baba yetu." (Kwa maana Manoa hakujua ya kuwa yule mgeni ni malaika wa Baba yetu.)
17Manoa akamwuliza malaika wa Baba yetu, "Jina lako ni nani, ili tukupe heshima maneno yako yatakapotimia?"
18Malaika wa Baba yetu akamwambia, "Kwa nini kuuliza jina langu? Nalo lapita akili."
19Basi Manoa akatwaa yule mwana-mbuzi pamoja na sadaka ya unga, akavitoa juu ya mwamba kwa Baba yetu, yeye afanyaye maajabu, huku Manoa na mkewe wakitazama. 20Ikawa, miali ya moto ilipopanda juu kutoka madhabahuni kuelekea mbinguni, malaika wa Baba yetu akapanda katika ule mwali wa madhabahu. Manoa na mkewe wakaona, wakaanguka kifudifudi hata nchi. 21Malaika wa Baba yetu hakumtokea tena Manoa na mkewe. Ndipo Manoa akajua ya kuwa alikuwa ni malaika wa Baba yetu. 22Manoa akamwambia mkewe, "Hakika tutakufa, kwa maana tumemwona Baba yetu!"
23Lakini mkewe akamwambia, "Kama Baba yetu angependa kutuua, asingalipokea sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya unga mikononi mwetu, wala asingalituonyesha haya yote, wala kutusikizisha mambo kama haya sasa." 24Yule mwanamke akazaa mwana, akamwita jina lake Samsoni. Mtoto akakua, naye Baba yetu akambariki. 25Roho wa Baba yetu akaanza kumsukuma huko Mahane-dani, kati ya Sora na Eshtaoli.