Baba Awakabidhi Israeli Mji wa Ai
8 1Kisha Baba yetu akamwambia Yoshua, "Usiogope wala usikate tamaa. Uwachukue watu wote wa vita pamoja nawe, upande Ai. Tazama, nimekutia mkononi mwako mfalme wa Ai, watu wake, mji wake, na nchi yake. 2Umtendee Ai na mfalme wake kama ulivyomtendea Yeriko na mfalme wake—ila nyara zake na wanyama wake mtajitwalia. Weka waviziao nyuma ya mji."
3Basi Yoshua na watu wote wa vita wakainuka kwenda Ai. Akachagua mashujaa hodari elfu thelathini, akawapeleka usiku. 4Akawaagiza, akisema, "Angalieni, mtavizia nyuma ya mji—msiwe mbali sana na mji. Nanyi nyote mwe tayari. 5Nami na watu wote nilio nao tutaukaribia mji. Nao watakapotoka kutupinga kama mara ya kwanza, tutakimbia mbele yao. 6Nao watatufuata hata tuwavute mbali na mji, kwa maana watasema, 'Wanatukimbia kama mara ya kwanza.' Basi tutakimbia mbele yao. 7Ndipo mtatoka mahali mlipovizia na kuuteka mji, kwa maana Baba yenu atautia mkononi mwenu. 8Nanyi mtakapokwisha kuuteka mji, mtauteketeza kwa moto. Fanyeni kama Baba yetu alivyoamuru. Angalieni, nimewaamuru."
9Basi Yoshua akawapeleka, nao wakaenda mahali pa kuvizia, wakakaa kati ya Betheli na Ai, upande wa magharibi wa Ai; lakini Yoshua akalala usiku ule kati ya watu. 10Yoshua akaamka asubuhi na mapema, akawakusanya watu, naye pamoja na wazee wa Israeli akawaongoza kupanda Ai. 11Watu wote wa vita waliokuwa pamoja naye wakainuka, wakasogea mbele hata wakafika mkabala wa mji, wakapiga kambi upande wa kaskazini wa Ai; palikuwa na bonde kati yao na Ai. 12Akatwaa kama watu elfu tano, akawaweka wavizie kati ya Betheli na Ai, upande wa magharibi wa mji. 13Basi wakawaweka watu, kambi yote iliyokuwa upande wa kaskazini wa mji, na waviziao wake upande wa magharibi wake; naye Yoshua akaenda usiku ule katikati ya bonde. 14Ikawa mfalme wa Ai alipoona hayo, watu wa mji wakaamka mapema, wakatoka haraka kupigana na Israeli, yeye na watu wake wote, mahali palipoamriwa, mkabala wa Araba; lakini hakujua ya kuwa palikuwa na waviziao nyuma ya mji. a a v14 Araba ni bonde refu la Yordani lililoshuka chini, likienda kusini kutoka Bahari ya Galilaya kuelekea Bahari ya Chumvi. 15Yoshua na Israeli wote wakajifanya kama walioshindwa mbele yao, wakakimbia kuelekea jangwani. 16Watu wote waliokuwa mjini wakaitwa ili wawafuatie; wakamfuatia Yoshua, wakavutwa mbali na mji. 17Hakubaki mtu ye yote katika Ai wala Betheli asiyetoka kuwafuatia Israeli; wakauacha mji wazi, wakawafuatia Israeli.
18Ndipo Baba yetu akamwambia Yoshua, "Nyosha mkuki ulio mkononi mwako kuuelekea Ai, kwa maana nitautia mkononi mwako." Basi Yoshua akaunyosha mkuki uliokuwa mkononi mwake kuuelekea mji.
19Mara alipouinua mkono wake, wale waviziao wakainuka upesi mahali pao, wakapiga mbio, wakaingia mjini, wakauteka, wakafanya haraka kuuteketeza mji kwa moto. 20Basi watu wa Ai wakageuka nyuma, wakatazama, na tazama, moshi wa mji ulikuwa ukipanda mbinguni, wala hawakuwa na nafasi ya kukimbilia huku wala huku; nao watu waliokimbilia jangwani wakawageukia wale waliowafuatia. 21Yoshua na Israeli wote walipoona ya kuwa wale waviziao wameuteka mji, na ya kuwa moshi wa mji unapanda, wakageuka nyuma, wakawapiga watu wa Ai. 22Nao wale wengine wakatoka mjini kuwaelekea; hivyo watu wa Ai wakawa katikati ya Israeli, wengine upande huu na wengine upande huu. Wakawapiga hata usibaki hata mmoja aliyesalia wala kuokoka. 23Lakini mfalme wa Ai wakamtwaa hai, wakamleta kwa Yoshua.
24Ikawa hapo Israeli walipokwisha kuwaua wenyeji wote wa Ai katika mashamba na jangwani mahali walipowafuatia, nao wote walipokwisha kuanguka kwa makali ya upanga hata wakaangamia, Israeli wote wakarudi Ai, wakaupiga kwa makali ya upanga. 25Nao wote walioanguka siku ile, waume kwa wake, walikuwa watu elfu kumi na mbili, ndio watu wote wa Ai. 26Kwa maana Yoshua hakuurudisha mkono wake aliouinua pamoja na mkuki, hata alipokwisha kuwaangamiza kabisa wenyeji wote wa Ai. 27Ila wanyama na nyara za mji ule Israeli wakajitwalia, kama Baba yetu alivyomwamuru Yoshua. 28Basi Yoshua akauteketeza Ai kwa moto, akaufanya kuwa chungu cha magofu milele, ukiwa hata leo hii. 29Naye akamtundika mfalme wa Ai mtini hata jioni; na jua lilipokuchwa Yoshua akaamuru maiti yake ishushwe kutoka mtini, wakaitupa penye maingilio ya lango la mji, wakainua juu yake chungu kikubwa cha mawe, kilichoko hata leo hii.
Israeli Wafanya Upya Agano la Baba
30Ndipo Yoshua akamjengea Baba yetu, Mungu wa Israeli, madhabahu katika Mlima Ebali, 31kama vile Musa, mtumishi wa Baba yetu, alivyowaamuru wana wa Israeli—kama ilivyoandikwa katika kitabu cha torati ya Musa—madhabahu ya mawe yasiyochongwa, ambayo hakuna mtu aliyeyagusa kwa chuma. Juu yake wakamtolea Baba yetu sadaka za kuteketezwa, na kutoa sadaka za amani. 32Hapo, mbele ya wana wa Israeli, akaandika juu ya mawe nakala ya torati ya Musa, aliyoiandika Musa. 33Israeli wote—mgeni na mzalia sawasawa—pamoja na wazee wao, na maakida, na waamuzi wao, wakasimama pande zote mbili za sanduku, wakiwaelekea makuhani Walawi waliolichukua sanduku la agano la Baba yetu. Nusu yao wakaelekea Mlima Gerizimu, na nusu wakaelekea Mlima Ebali, kama vile Musa, mtumishi wa Baba yetu, alivyoamuru tangu awali, ili kuwabariki watu wa Israeli. 34Kisha akasoma maneno yote ya torati, baraka na laana, sawasawa kabisa na yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati. 35Hapana neno lo lote katika yale yote aliyoamuru Musa ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya kusanyiko lote la Israeli, pamoja na wanawake, na watoto, na wageni waliokaa kati yao.