Soma. Pokea. Pendekeza.

♥ Maoni

Yoshua 5

Kitabu

Baba Awafanya Upya Watu Wake huko Gilgali

Sura ya 5.

Ikawa wafalme wote wa Waamori waliokuwa upande wa magharibi wa Yordani, na wafalme wote wa Wakanaani waliokuwa kando ya bahari, waliposikia ya kwamba Baba yetu ameyakausha maji ya Yordani mbele ya Israeli hata wakavuka, mioyo yao ikayeyuka, wala haikubaki roho ndani yao kwa sababu ya wana wa Israeli.

Wakati ule Baba yetu akamwambia Yoshua, "Jifanyie visu vya mawe, ukawatahiri wana wa Israeli tena mara ya pili."

Basi Yoshua akajifanyia visu vya mawe, akawatahiri wana wa Israeli hapo Gibeath-haaralothi, yaani Kilima cha Magovi. Na sababu ya Yoshua kuwatahiri ndiyo hii: watu wote waliotoka Misri, yaani wanaume, watu wote wa vita, walikuwa wamekufa jangwani njiani, walipokwisha kutoka Misri. Kwa maana watu wote waliotoka walikuwa wametahiriwa, bali watu wote waliozaliwa jangwani njiani walipotoka Misri hawakuwa wametahiriwa. Kwa kuwa wana wa Israeli walitembea miaka arobaini jangwani, hata taifa lote, watu wa vita waliotoka Misri, walipokwisha kuangamia, kwa sababu hawakuitii sauti ya Baba yetu; ambao Baba yetu aliwaapia ya kwamba hatawaacha waione nchi ile aliyowaapia baba zao kutupa sisi, nchi ijaayo maziwa na asali. Naye akawainua watoto wao mahali pao, nao ndio Yoshua aliowatahiri; kwa maana walikuwa hawajatahiriwa, kwa sababu hawakuwa wametahiriwa njiani. Ikawa walipokwisha kutahiriwa taifa lote, walikaa mahali pao kambini hata walipopona.

Kisha Baba yetu akamwambia Yoshua, "Leo nimeivingirisha aibu ya Misri iondoke kwenu." Kwa hiyo mahali pale pakaitwa Gilgali hata leo.

Wana wa Israeli wakapiga kambi huko Gilgali; wakaifanya Pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi, jioni, katika nchi tambarare za Yeriko. Wakala mazao ya nchi siku ya pili baada ya Pasaka, siku iyo hiyo, mikate isiyotiwa chachu, na bisi. Ile mana ikakoma siku ya pili baada ya kula mazao ya nchi; wana wa Israeli hawakuwa na mana tena, bali wakala matunda ya nchi ya Kanaani mwaka ule.

Jemadari wa Jeshi la Baba

Ikawa Yoshua alipokuwa karibu na Yeriko, akainua macho yake akaona, na tazama, mtu amesimama mbele yake, na upanga wake mkononi mwake umefutwa alani. Yoshua akamwendea, akamwuliza, "Je! Wewe u upande wetu, au upande wa adui zetu?"

Akasema, "La; bali nimekuja sasa nikiwa jemadari wa jeshi la Baba yetu." Yoshua akaanguka kifudifudi hata nchi, akasujudu, akamwambia, "Bwana wangu ana neno gani kwa mtumishi wake?"

Yule jemadari wa jeshi la Baba yetu akamwambia Yoshua, "Vua viatu vyako miguuni mwako, kwa maana mahali unaposimama ni patakatifu." Yoshua akafanya vivyo.

A young man reading the Father's Heart Bible print edition in a coffee shop Sasa Imechapishwa

Maoni

Mawazo, maswali, au neno ambalo sura hii imeliamsha ndani yako — lishiriki hapa. Kila maoni huweka jina lako kwenye Wall of Contributors.

Kusoma, kunakili na kushiriki ni wazi kwa kila mtu — huhitaji akaunti. Kutoa maoni, kutia alama, na kuhifadhi mahali ulipofikia hupatikana kwa akaunti ya bure, na kila maoni huweka jina lako kwenye Wall of Contributors.

Jiunge na Familia — ni bure →
  • Bado hakuna maoni. Kuwa wa kwanza kuchangia.