Yoshua Awaita Israeli Washikamane na Baba
23 1Muda mrefu baada ya Baba yetu kuwapa Israeli raha kutoka kwa adui zao wote waliowazunguka, Yoshua alikuwa mzee, ameingia sana miakani. 2Yoshua akawaita Israeli wote—wazee, vichwa, waamuzi, na maakida—akawaambia, "Mimi ni mzee, nimeingia sana miakani. 3Ninyi mmeona yote Baba yenu aliyowatendea mataifa haya yote kwa ajili yenu; Baba yenu ndiye aliyewapigania. 4Tazameni, nimewagawia, kuwa urithi kwa kabila zenu, mataifa haya yaliyobaki, pamoja na mataifa yote niliyoyakatilia mbali, kutoka Yordani hata Bahari Kuu upande wa magharibi. 5Baba yenu mwenyewe atawasukuma nyuma na kuwafukuza mbele yenu, nanyi mtaimiliki nchi yao, kama Baba yenu alivyowaahidi.
6Basi kuweni hodari sana kushika na kutenda yote yaliyoandikwa katika kitabu cha sheria ya Musa, msiache kuiacha kwa kuelekea kuume wala kushoto. 7Msichanganyike na mataifa haya yaliyobaki katikati yenu. Msiyataje majina ya miungu yao wala kuapa kwao; msiwatumikie wala kuwasujudia. 8Bali shikamaneni na Baba yenu, kama mlivyofanya hata leo hii.
9Baba yenu amewafukuza mbele yenu mataifa makubwa na yenye nguvu; hakuna mtu aliyeweza kusimama mbele yenu hata leo hii. 10Mtu mmoja miongoni mwenu huwafukuza watu 1,000, kwa maana Baba yenu mwenyewe ndiye awapiganiaye, kama alivyowaahidi. 11Basi jihadharini sana nafsi zenu, mpate kumpenda Baba yenu. 12Lakini kama mkigeuka na kushikamana na mataifa haya yaliyobaki katikati yenu, mkaoana nao, mkichanganyika nao nao pamoja nanyi, 13jueni hakika ya kuwa Baba yenu hataendelea kuyafukuza mataifa haya mbele yenu. Yatakuwa mtego na tanzi kwenu, mjeledi mbavuni mwenu na miiba machoni penu, hata mtakapoangamia katika nchi hii njema Baba yenu aliyowapa.
14Sasa mimi naenda njia ya dunia yote. Nanyi mnajua kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote ya kuwa hakuna hata neno moja jema kati ya yote Baba yenu aliyoyaahidi juu yenu lililopungua—yote yamewatimilikia; hakuna hata moja lililopungua. 15Basi kama vile kila neno jema Baba yenu alilowaambia lilivyowatimilikia, ndivyo atakavyoyaleta juu yenu kila neno baya, hata atakapowaangamiza katika nchi hii njema aliyowapa. 16Mkilivunja agano la Baba yenu, aliyowaamuru, mkaenda kuitumikia miungu mingine na kuisujudia, hasira ya Baba yenu itawaka juu yenu, nanyi mtaangamia upesi katika nchi njema aliyowapa."