Ni Nani Aliyemwacha Punda-mwitu Huru?
39 1"Je, wajua wakati mbuzi wa mlimani wanapozaa? Je, waziangalia paa wanapozaa? 2Je, waweza kuhesabu miezi wanayochukua mimba? Je, wajua wakati wanapozaa? 3Hujiinamisha na kuzaa; uchungu wao wa kuzaa umekwisha. 4Watoto wao hukua na kuwa na nguvu kondeni; huondoka wala hawarudi.
5"Ni nani aliyemwacha punda-mwitu huru? Ni nani aliyezifungua kamba za punda mwepesi, 6ambaye nimempa jangwa liwe makao yake na nchi ya chumvi iwe maskani yake? 7Huzidharau kelele za mji wala hasikii ukelele wa mwendesha-punda. 8Hutanga-tanga milimani kutafuta malisho yake, akitafuta kila kitu cha kijani.
9"Je, nyati yu radhi kukutumikia? Je, atalala usiku kando ya hori lako la kulishia? 10Je, waweza kumfunga nyati kwenye mtaro kwa kamba? Je, atalima mabondeni nyuma yako? 11Je, utamtegemea kwa sababu nguvu zake ni nyingi? Je, utamwachia kazi yako? 12Je, waweza kumwamini akurudishie nafaka yako na kuikusanya kwenye sakafu yako ya kupuria?
13"Mbawa za mbuni hupiga-piga kwa furaha, lakini je, ni manyoya na uzuri wa korongo? 14Huyaacha mayai yake juu ya ardhi na kuyaacha yapate joto mavumbini, 15akisahau kwamba mguu waweza kuyaponda, au mnyama wa mwitu aweza kuyakanyaga. 16Huwatenda watoto wake kwa ukatili, kana kwamba si wake mwenyewe; haogopi kwamba taabu yake imekuwa bure, 17kwa sababu nilimsahaulisha hekima wala sikumpa fungu katika ufahamu. 18Lakini akianza kupiga mbio, humcheka farasi na mpanda-farasi wake.
19"Je, wewe humpa farasi nguvu zake? Je, waivika shingo yake manyoya yanayopepea? 20Je, wamfanya arukaruke kama nzige? Mlio wa pua yake wa fahari huleta hofu. 21Hupiga-piga miguu bondeni na kufurahia nguvu zake; hukimbilia vitani. 22Huicheka hofu wala haogopi; harudi nyuma mbele ya upanga. 23Podo hutagatanya juu yake, mkuki unaong'aa na fumo. 24Kwa shauku kali na ya hasira huila ardhi; hawezi kusimama tuli tarumbeta ilipolia. 25Kila tarumbeta ilipolia husema, 'Aha!' Huisikia harufu ya vita kutoka mbali, ngurumo ya majemadari na kelele ya vita.
26"Je, ni kwa ufahamu wako kwamba kipanga huruka na kutandaza mbawa zake kuelekea kusini? 27Je, ni kwa amri yako kwamba tai hupaa juu na kujenga kiota chake mahali pa juu? 28Hukaa juu ya jabali na kufanya maskani yake humo, juu ya mwamba wenye majabali, ngome yake. 29Kutoka huko hutafuta chakula chake; macho yake hukiona kutoka mbali sana. 30Makinda yake hujilisha damu, na palipo na waliouawa, ndipo yeye alipo."