Bildadi Anena Tena
18 1Ndipo Bildadi, Mshuhi, akajibu: 2"Hata lini utawinda maneno? Onyesha akili kidogo, kisha tuweze kuzungumza. 3Kwa nini tunachukuliwa kama ng'ombe, tunahesabiwa kuwa wapumbavu machoni pako? 4Wewe unayejirarua vipande kwa hasira yako—je, dunia iachwe kwa ajili yako, au mwamba uondolewe mahali pake? 5Naam, nuru ya mwovu huzimwa, na mwali wa moto wake hutiwa giza. 6Nuru hutiwa giza katika hema lake, na taa iliyo juu yake huzimika. 7Hatua zake za nguvu hukatizwa, na mipango yake mwenyewe humwangusha chini. 8Miguu yake mwenyewe humwingiza katika wavu, naye hutembea moja kwa moja ndani ya matundu yake. 9Mtego humkamata kisigino; tanzi humshika kwa nguvu. 10Kitanzi kimefichwa kwa ajili yake ardhini, na mtego umewekwa ukimngoja njiani mwake. 11Vitisho humshtua pande zote na kumfukuza visigino mwake. 12Nguvu zake hudhoofishwa kwa njaa, na maafa yasimama tayari kwa anguko lake. 13Huila vipande vya ngozi yake; mzaliwa wa kwanza wa mauti huila viungo vyake. a a v13 "Mzaliwa wa kwanza wa mauti" ni usemi wa kishairi kuelezea ugonjwa hatari unaodhoofisha—wakala hatari zaidi wa mauti. 14Hung'olewa kutoka usalama wa hema lake na kupelekwa kwa mfalme wa vitisho. 15Moto hukaa katika hema lake, lisilo lake tena; kiberiti kiwakacho hutawanywa juu ya makao yake. 16Mizizi yake hukauka chini, na matawi yake hunyauka juu. 17Kumbukumbu yake hutoweka duniani, wala hana jina barabarani. 18Hufukuzwa kutoka nuruni hadi gizani na kufurushwa nje ya ulimwengu. 19Haachi mzao wala uzao miongoni mwa watu wake, wala aliyesalia mahali alipokaa hapo awali. 20Wale wa magharibi hushangaa kwa hatima yake, na wale wa mashariki hushikwa na hofu. 21Hakika ndivyo huwa makao ya waovu, mahali pa yule asiyemjua Mungu."