Uchungu wa Nafsi
10 1"Nimeuchukia uhai wangu mwenyewe. Nitaachilia kilio changu kiende bila kizuizi; nitanena kwa uchungu wa nafsi yangu. 2Nitamwambia Mungu: Usinihukumu kuwa mwenye hatia; nijulishe kwa nini unashindana nami. 3Je, unafurahia kudhulumu, kuidharau kazi ya mikono yako, huku ukiitabasamia mipango ya waovu? 4Je, wewe una macho ya nyama? Je, wewe waona kama binadamu aonavyo? 5Je, siku zako ni kama siku za binadamu, au miaka yako ni kama miaka ya mtu, 6hata ukatafute uovu wangu na kuwinda dhambi yangu, 7ingawa unajua ya kuwa mimi si mwenye hatia, wala hakuna awezaye kuniokoa kutoka mkononi mwako?
8"Mikono yako ilinifinyanga na kunifanya, kila sehemu yangu, na sasa wageuka na kuniangamiza. 9Kumbuka ya kuwa ulinifinyanga kama udongo. Je, sasa utanirudisha mavumbini? 10Je, hukunimimina kama maziwa na kunigandamiza kama jibini, 11ukanivika ngozi na nyama, na kuniunga pamoja kwa mifupa na mishipa? 12Ulinipa uhai na upendo wa agano, na uangalizi wako umeilinda roho yangu.
13"Lakini uliyaficha haya moyoni mwako, nami najua ya kuwa hii ndiyo ilikuwa nia yako: 14kama ningetenda dhambi, ungekuwa ukiniangalia na usingeniachilia na hatia yangu. 15Kama mimi ni mwenye hatia, ole wangu! Na hata kama sina hatia, siwezi kuinua kichwa changu—nimejaa aibu, nimezama katika mateso yangu. 16Kama nikiinua kichwa changu juu, unaniwinda kama simba na tena wafanya maajabu dhidi yangu. 17Waleta mashahidi wapya dhidi yangu na kumwaga zaidi ya ghadhabu yako juu yangu; wimbi baada ya wimbi la taabu lanishambulia.
18"Kwa nini basi ulinitoa tumboni? Ningetamani ningekufa kabla ya jicho lolote kuniona. 19Ningekuwa kama vile sikuwahi kuwako kamwe, nikichukuliwa moja kwa moja kutoka tumboni hadi kaburini. 20Je, siku zangu si chache? Niachie mbali nami, niache peke yangu, ili nipate muda kidogo wa faraja, 21kabla sijaenda mahali pasipo na kurudi, hadi nchi ya giza na kivuli kizito, 22hadi nchi ya utusitusi kama usiku wa manane, ya kivuli kizito na machafuko, ambako hata nuru ni kama giza."