Shuka Chini, Binti Babeli
Binti Babeli anaambiwa ashuke kutoka kiti chake cha enzi, achukue jiwe la kusagia la mtumwa, na akae mavumbini. Baba yetu alimtumia kuiadhibu Israeli, lakini hakuonyesha huruma hata kwa wazee, akajiambia kwamba hakuna aliyeona. Wanajimu wake wanaungua kama mabua; hakuna wa kumwokoa.
47 1"Shuka chini, keti mavumbini, ewe bikira binti Babeli; keti chini ardhini, bila kiti cha enzi, ewe binti wa Wakaldayo. Hawatakuita tena mpole na mwororo.
2"Chukua mawe ya kusagia, usage unga; ondoa utaji wako, vua vazi lako, funua miguu yako, vuka mito. 3Uchi wako utafunuliwa, na aibu yako itaonekana. Nitaleta haki, wala sitamhurumia mtu yeyote."
4Mkombozi wetu—Baba wa majeshi ya mbinguni ndilo jina lake— Mtakatifu wa Israeli, Baba yetu.
5Keti kimya, na uingie gizani, ewe binti wa Wababeli; kwa maana hutaitwa tena malkia wa falme. 6Niliwakasirikia watoto wangu; niliunajisi urithi wangu, nikawatia mkononi mwako. Hukuwaonyesha rehema; hata kwa wazee uliweka nira nzito sana. 7Ulisema, "Nitakuwa malkia milele"—kwa hiyo hukuyatia moyoni mambo haya wala hukukumbuka jinsi yatakavyoishia.
8Basi sasa, sikiliza hili, ewe upendaye anasa, uketiye salama, useme moyoni mwako, "Mimi ndimi, wala hakuna mwingine ila mimi; sitaketi kamwe kama mjane wala sitajua kufiwa na watoto." 9Lakini mambo haya mawili yatakujia kwa dakika moja, katika siku moja: kufiwa na watoto na ujane. Yatakujia kwa kipimo kilichojaa, licha ya uchawi wako mwingi na nguvu kubwa ya maganga yako.
10Uliutumaini uovu wako mwenyewe; ulisema, 'Hakuna anionaye.' Hekima yako na maarifa yako yalikupotosha, hata ukafikiri, 'Mimi peke yangu ndimi, wala hakuna mwingine ila mimi.' 11Kwa hiyo msiba utakujia usioujua jinsi ya kuuloga uondoke; maafa yatakuangukia usiyoweza kuyakinga; uharibifu utakujia ghafula, kabla hujajua.
12Basi endelea na maganga yako na uchawi wako mwingi ambao umejishughulisha nao tangu ujana wako. Labda utafanikiwa; labda utaleta hofu. 13Umechoka kwa mashauri yako mengi. Na wasimame basi wakuokoe— wale wanaochora ramani ya mbingu, wanaotazama nyota, wanaobashiri kila mwezi mpya yatakayokujia. 14Tazama, wako kama makapi; moto huwateketeza. Hawawezi kujiokoa nafsi zao kutoka nguvu ya mwali. Haya si makaa ya kuota moto, wala si moto wa kuketi karibu nao. 15Hivi ndivyo walivyo kwako—wale uliofanya nao kazi na biashara tangu ujana wako. Kila mmoja hutangatanga kwa njia yake mwenyewe; hakuna wa kukuokoa.