Kuitwa kwa Abramu
12 1Basi Baba yetu akamwambia Abramu, "Toka katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha. 2Nami nitakufanya kuwa taifa kubwa, nami nitakubariki; nitalikuza jina lako, nawe utakuwa baraka. 3Nitawabariki wakubarikio, na yeyote akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia zitabarikiwa." a a v3 Paulo anaita mstari huu injili iliyohubiriwa kwa Abrahamu mapema — kila jamaa duniani ikibarikiwa kwa njia yake, ikitimizwa katika Yesu (Wagalatia 3:8).
4Abramu akaenda kama Baba yetu alivyomwambia, na Lutu akaenda pamoja naye. Abramu alikuwa na miaka sabini na mitano alipoondoka Harani. 5Abramu akamchukua Sarai mkewe, na Lutu mwana wa ndugu yake, na mali yote waliyokuwa wamekusanya, na watu waliowapata huko Harani, wakatoka kwenda nchi ya Kanaani, wakafika nchi ya Kanaani. 6Abramu akapita katika nchi hiyo mpaka mahali pa Shekemu, mpaka mwaloni wa More. Wakati huo Wakanaani walikuwa katika nchi ile.
7Ndipo Baba yetu akamtokea Abramu, akasema, "Nchi hii nitawapa wazao wako." Basi Abramu akamjengea Baba yetu madhabahu huko, yeye aliyemtokea. b b v7 Paulo anasoma neno "mzao" hapa kuwa mzao mmoja — Yesu — ambaye kwa njia yake baraka ya Abrahamu inafikia kila taifa (Wagalatia 3:16).
8Kutoka huko akahamia nchi ya milima upande wa mashariki wa Betheli, akapiga hema yake, Betheli upande wa magharibi, na Ai upande wa mashariki. Akamjengea Baba yetu madhabahu huko, akaliitia jina la Baba yetu. 9Kisha Abramu akaendelea na safari yake, akielekea Negebu.
Njaa na Njia ya Kwenda Misri
10Kwa kuwa njaa iliipata nchi, Abramu akashuka mpaka Misri ili akae huko, kwa maana njaa ilikuwa kali katika nchi. 11Alipokaribia kuingia Misri, akamwambia Sarai mkewe, "Najua ya kuwa wewe ni mwanamke mzuri wa sura. 12Wamisri watakapokuona, watasema, 'Huyu ni mkewe,' nao wataniua mimi, bali wewe watakuacha hai. 13Tafadhali sema ya kuwa u dada yangu, ili niwe salama kwa ajili yako, na nafsi yangu ihifadhiwe hai kwa sababu yako."
14Ikawa Abramu alipoingia Misri, Wamisri wakamwona yule mwanamke ya kuwa ni mzuri sana wa sura. 15Maakida wa Farao wakamwona, wakamsifu mbele ya Farao; naye yule mwanamke akachukuliwa nyumbani mwa Farao. 16Naye akamtendea Abramu mema kwa ajili yake, Abramu akapata kondoo, na ng'ombe, na punda waume na wake, na watumishi waume na wake, na ngamia. 17Lakini Baba yetu akampiga Farao na nyumba yake kwa mapigo makuu kwa sababu ya Sarai, mke wa Abramu. 18Farao akamwita Abramu, akasema, "Ni nini hili ulilonitendea? Mbona hukuniambia ya kuwa ni mkeo? 19Mbona ulisema, 'Ni dada yangu,' hata nikamchukua awe mke wangu? Basi sasa, hapa ndiye mkeo—mchukue, uende zako."
20Farao akawaagiza watu wake juu ya Abramu, nao wakamsindikiza, yeye na mkewe, na yote aliyokuwa nayo.