Baba Achochea Moyo wa Mfalme
1 1Katika mwaka wa kwanza wa Koreshi mfalme wa Uajemi, ili kulitimiza neno la Baba yetu lililonenwa kwa kinywa cha Yeremia, Baba yetu aliichochea roho ya Koreshi mfalme wa Uajemi, hata akapiga mbiu katika ufalme wake wote, tena akaiandika, akisema:
2Koreshi mfalme wa Uajemi asema hivi: "BWANA, Mungu wa mbinguni, amenipa falme zote za dunia, naye ameniagiza nimjengee nyumba huko Yerusalemu katika Yuda. 3Kila mtu miongoni mwenu katika watu wake wote—Mungu wake na awe pamoja naye—na apande kwenda Yerusalemu katika Yuda, akaijenge upya nyumba ya BWANA, Mungu wa Israeli; yeye ndiye Mungu aliye katika Yerusalemu. 4Na kila mtu aliyesalia, popote akaapo, na asaidiwe na watu wa mahali pake kwa fedha, na dhahabu, na mali, na wanyama, pamoja na sadaka za hiari kwa ajili ya nyumba ya Mungu iliyoko Yerusalemu."
5Ndipo wakuu wa jamaa za Yuda na Benyamini, na makuhani, na Walawi—kila mtu ambaye Baba yetu alikuwa ameichochea roho yake—wakainuka ili wapande kwenda kuijenga upya nyumba ya Baba yetu iliyoko Yerusalemu. 6Na jirani zao wote wakawategemeza kwa vyombo vya fedha na dhahabu, na kwa mali, na wanyama, na vitu vya thamani, mbali na vyote vilivyotolewa kwa hiari.
7Mfalme Koreshi naye akavitoa vyombo vya nyumba ya Baba yetu, ambavyo Nebukadneza alivichukua kutoka Yerusalemu na kuviweka katika nyumba ya miungu yake. 8Koreshi mfalme wa Uajemi akaviondoa kwa mkono wa Mithredathi mtunza-hazina, akavihesabu na kumkabidhi Sheshbaza mkuu wa Yuda. 9Na hii ndiyo hesabu yake: mabakuli ya dhahabu thelathini, mabakuli ya fedha elfu moja, visahani vya kufukizia uvumba ishirini na tisa, 10mabakuli mengine ya dhahabu thelathini, mabakuli mengine ya fedha ya namna nyingine mia nne na kumi, na vyombo vingine elfu moja. 11Vyombo vyote vya dhahabu na fedha vilikuwa elfu tano na mia nne. Sheshbaza akavipandisha vyote hivyo hapo wale waliokuwa uhamishoni walipopanda kutoka Babeli kwenda Yerusalemu.