Kitabu cha Kukunjwa Kitamu kama Asali
Anakula gombo nalo ni tamu kama asali, kisha anachukuliwa hadi kwa waliohamishwa huko Tel-abibu, ambako anaketi kati yao siku saba akiwa ameshangaa. Baba yetu anamfanya mlinzi, mwenye kuwajibika kuonya, kisha anaufunga ulimi wake ili aseme tu anapopewa maneno.
3 1Akaniambia, "Mwana wa Adamu, kula unachokipata. Kula kitabu hiki cha kukunjwa, kisha uende ukaseme na nyumba ya Israeli."
2Basi nikafungua kinywa changu, naye akanipa kitabu hiki cha kukunjwa nikale.
3Akaniambia, "Mwana wa Adamu, lisha tumbo lako na ujaze matumbo yako kwa kitabu hiki cha kukunjwa ninachokupa." Nikakila, nacho kinywani mwangu kilikuwa kitamu kama asali.
4Kisha akaniambia, "Mwana wa Adamu, nenda kwa nyumba ya Israeli ukaseme nao maneno yangu.
5"Kwa maana hukutumwa kwa watu wenye usemi usioeleweka na lugha ngumu, bali kwa nyumba ya Israeli, 6wala si kwa mataifa mengi yenye usemi usioeleweka na lugha ngumu, ambao maneno yao huwezi kuyaelewa. Hakika, kama ningekutuma kwao, wangekusikiliza. 7Lakini nyumba ya Israeli haitakubali kukusikiliza, kwa sababu hawakubali kunisikiliza mimi; kwa maana nyumba yote ya Israeli wana vichwa vigumu na mioyo migumu. 8Tazama, nimeufanya uso wako kuwa mgumu kama nyuso zao, na kipaji chako cha uso kuwa kigumu kama vipaji vyao vya uso. 9Nimekifanya kipaji chako cha uso kama almasi, kigumu kuliko gumegume. Usiwaogope wala usifadhaishwe na sura zao, kwa maana ni nyumba ya kuasi."
10Akaniambia, "Mwana wa Adamu, yapokee moyoni mwako maneno yangu yote ninayonena nawe, na uyasikie kwa masikio yako. 11Nenda kwa watu waliohamishwa, watu wako mwenyewe, ukaseme nao. Waambie, 'Bwana Baba Mwenye Enzi asema hivi,' wakisikiliza au wakikataa kusikiliza."
12Kisha Roho wa Baba yetu akaniinua, na nyuma yangu nikasikia sauti kuu ya mvumo: "Utukufu wa Baba yetu na uhimidiwe kutoka mahali pake pa kukaa!" 13sauti ya mabawa ya wale wenye uhai yakigusana, na sauti ya magurudumu yaliyokuwa kando yao, sauti ya mvumo mkuu. 14Roho akaniinua na kunichukua, nami nikaenda nikiwa na uchungu, roho yangu ikiwaka ndani yangu, mkono wa Baba yetu ukiwa na nguvu juu yangu. 15Nikafika kwa watu waliohamishwa huko Tel-abibu kando ya mto Kebari, nami nikaketi kati yao pale, nimeshangaa, siku saba.
Baba Amweka Mlinzi
16Mwisho wa siku saba, neno la Baba yetu likanijia:
17"Mwana wa Adamu, nimekufanya kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli. Utakaposikia neno kutoka kinywani mwangu, waonye kutoka kwangu. 18Nikimwambia mtu mwovu, 'Hakika utakufa,' nawe usimwonye wala usinene kumwonya huyo mwovu aiache njia yake mbaya ili kuiokoa nafsi yake, huyo mwovu atakufa kwa dhambi yake, lakini nitaidai damu yake mkononi mwako.
19"Lakini ukimwonya huyo mwovu naye asigeuke kuiacha njia yake mbaya, atakufa kwa dhambi yake, bali wewe utakuwa umeiokoa nafsi yako.
20"Tena, mtu mwenye haki agebeukapo kuiacha haki yake na kutenda mabaya, nami nikiweka kizuizi mbele yake, atakufa. Kwa kuwa hukumwonya, atakufa kwa dhambi yake, na matendo yake ya haki hayatakumbukwa, nami nitaidai damu yake mkononi mwako. 21Lakini ukimwonya mtu mwenye haki asitende dhambi, naye asitende, ataishi kwa sababu alikubali onyo, nawe utakuwa umeiokoa nafsi yako."
22Mkono wa Baba yetu ulikuwa juu yangu pale, naye akaniambia, "Inuka, toka nje uende bondeni, nami nitasema nawe huko."
23Basi nikainuka nikaenda bondeni, na tazama, utukufu wa Baba yetu ulisimama pale, kama ule utukufu niliouona kando ya mto Kebari, nami nikaanguka kifudifudi.
24Roho akaingia ndani yangu, akanisimamisha kwa miguu yangu, akasema nami, akaniambia: "Nenda, ukajifungie ndani ya nyumba yako. 25Nawe, mwana wa Adamu, tazama, watakufunga kamba juu yako na kukufunga nazo, hata usiweze kutoka nje kati ya watu.
26Nami nitaufanya ulimi wako ushikamane na kaakaa la kinywa chako; utakuwa bubu, usiweze kuwakemea, kwa maana ni nyumba ya kuasi. 27Lakini nitakaponena nawe, nitakifungua kinywa chako, nawe utawaambia, 'Bwana Baba Mwenye Enzi asema hivi.' Yeye atakayesikiliza, na asikilize; naye atakayekataa, na akatae—kwa maana ni nyumba ya kuasi."