Madhabahu ya Sadaka ya Kuteketezwa
38 1Akaifanya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa kwa mbao za mshita: urefu na upana wapata futi saba na nusu—mraba—na kwenda juu futi nne na nusu. 2Akafanya pembe katika pembe zake nne, zikawa kitu kimoja nayo, akaifunika kwa shaba. 3Akafanya vyombo vyote vya madhabahu: masufuria, majembe, mabakuli, uma, na vyetezo—vyombo vyake vyote kwa shaba. 4Akaifanyia madhabahu wavu wa shaba chini ya ukingo wake, ukafika hata katikati yake. 5Akasubu pete nne katika pembe nne za huo wavu wa shaba, ziwe mahali pa kutilia miti. 6Akaifanya miti kwa mbao za mshita, akaifunika kwa shaba. 7Akaitia hiyo miti katika zile pete pande za madhabahu, ili kuichukua kwayo; akaifanya ya vibao, yenye uvungu ndani.
Birika la Shaba
8Akalifanya birika la shaba na tako lake la shaba kwa vioo vya wanawake waliohudumu penye mlango wa hema ya kukutania.
9Akaifanya behewa. Pazia zake upande wa kusini zilikuwa za kitani nzuri iliyosokotwa, urefu wapata futi 150.
10Nguzo zake ishirini na matako yake ishirini: shaba. Kulabu za nguzo na tepe zake: fedha. 11Upande wa kaskazini: pazia za futi 150, pamoja na nguzo ishirini za shaba na matako ishirini ya shaba; kulabu za nguzo na tepe zake zilikuwa za fedha. 12Upande wa magharibi: pazia zapata futi sabini na tano, nguzo kumi, matako kumi; kulabu za nguzo na tepe zake zilikuwa za fedha. 13Upande wa mashariki, kuelekea mawio ya jua, behewa ilikuwa na upana wapata futi sabini na tano. 14Pazia za urefu wa futi ishirini na mbili na nusu upande mmoja wa lango, pamoja na nguzo tatu na matako matatu. 15Vivyo hivyo upande wa pili: pazia pande zote mbili za lango la behewa, urefu wapata futi ishirini na mbili na nusu, pamoja na nguzo tatu na matako matatu kila upande. 16Pazia zote zilizoizunguka behewa zilikuwa za kitani nzuri iliyosokotwa. 17Matako ya nguzo za behewa yalikuwa ya shaba; kulabu zake na tepe zake zilikuwa za fedha; kufunikwa kwa vichwa vyake kulikuwa kwa fedha; nguzo zote za behewa zilikuwa na tepe za fedha. 18Pazia la lango la behewa lilikuwa la kazi ya taraza kwa nyuzi za rangi ya samawati, ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri iliyosokotwa—urefu wapata futi thelathini, kwenda juu futi saba na nusu, kama pazia za behewa. 19Nguzo zake nne na matako yake manne yalikuwa ya shaba; kulabu zake, fedha; kufunikwa kwa vichwa vyake na tepe zake, fedha. 20Vigingi vyote vya maskani na vya kuizunguka behewa vilikuwa vya shaba.
Bezaleli na Oholiabu
21Hii ndiyo hesabu ya vitu vya maskani, maskani ya ushuhuda, kama ilivyohesabiwa kwa amri ya Musa—kazi ya Walawi chini ya Ithamari mwana wa Haruni kuhani. 22Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda, akafanya yote Baba yetu aliyomwamuru Musa, 23pamoja naye alikuwa Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani, mchongaji, mbunifu, na mtarizi kwa nyuzi za rangi ya samawati, ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri.
24Dhahabu yote iliyotumika katika kazi hiyo, katika kazi yote ya patakatifu—dhahabu ya sadaka ya kutikiswa—ilikuwa na uzito wapata ratili 2,193, kwa shekeli ya patakatifu. 25Fedha ya wale waliohesabiwa katika mkutano ilikuwa na uzito wapata ratili 7,545, kwa shekeli ya patakatifu: 26Wapata sehemu ya tano ya wakia ya fedha kwa kila mtu, kwa kila aliyehesabiwa, mwenye umri wa miaka ishirini na zaidi: watu 603,550. 27Wapata ratili 7,500 za fedha zilisubu matako ya patakatifu na matako ya pazia—matako mia moja kutokana na fedha hiyo, wapata ratili 75 kila moja. 28Kutokana na zile ratili arobaini na tano za fedha akafanya kulabu za nguzo, akafunika vichwa vyake, na kuzifanyia tepe. 29Shaba ya sadaka ya kutikiswa ilikuwa na uzito wapata ratili 5,310. 30Kwa hiyo akafanya matako ya mlango wa hema ya kukutania, madhabahu ya shaba pamoja na wavu wake wa shaba, na vyombo vyote vya madhabahu. 31Matako ya kuizunguka behewa, matako ya lango la behewa, vigingi vyote vya maskani, na vigingi vyote vya kuizunguka behewa.