Wana wa Yakobo huko Misri
1 1Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli waliokuja Misri pamoja na Yakobo, kila mmoja na jamaa yake: 2Reubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda, 3Isakari, Zabuloni, na Benyamini, 4Dani na Naftali, Gadi na Asheri. 5Wote waliozaliwa katika ukoo wa Yakobo walikuwa watu sabini; Yusufu alikuwa tayari yuko Misri. 6Kisha Yusufu akafa, na ndugu zake wote, na kizazi kile chote. 7Lakini watu wa Israeli wakazaana, wakaenea, wakaongezeka, na kuwa hodari mno, hata nchi ikajaa nao.
8Basi akatokea mfalme mpya katika Misri, ambaye hakumjua Yusufu. 9Akawaambia watu wake, "Tazameni, watu wa Israeli ni wengi na wenye nguvu kuliko sisi. 10Njoni, tuwatendee kwa hekima, wasije wakaongezeka, na ikitokea vita, wakaungana na adui zetu, wakapigana nasi, na kuiacha nchi." 11Kwa hiyo wakawawekea wasimamizi wa kazi ili kuwatesa kwa kazi ngumu ya kulazimishwa, wakijenga miji ya ghala ya Farao: Pithomu na Ramesesi. 12Lakini kadiri Wamisri walivyowaonea, ndivyo watu wa Israeli walivyozidi kuongezeka na kuenea, hata Wamisri wakawaogopa watu wa Israeli. 13Basi Wamisri wakawatumikisha watu wa Israeli kwa ukatili. 14Wakafanya maisha yao kuwa machungu kwa kazi ngumu ya kufinyanga chokaa na kufyatua matofali na kila aina ya kazi za shambani. Katika kazi zao zote ngumu Wamisri waliwatumikisha kwa ukatili.
15Kisha mfalme wa Misri akawaambia wakunga wa Kiebrania, mmoja aliyeitwa Shifra na mwingine Pua, 16"Mnapowasaidia wanawake wa Kiebrania kuzaa, angalieni katika kiti cha kuzalia: kama ni mtoto wa kiume, muueni; lakini kama ni wa kike, mwacheni aishi." 17Lakini wakunga wakamcha Baba yetu wa mbinguni, wala hawakufanya kama mfalme wa Misri alivyowaamuru; wakawaacha watoto wa kiume waishi. 18Basi mfalme wa Misri akawaita wale wakunga, akawaambia, "Kwa nini mmefanya jambo hili, mkiwaacha watoto wa kiume waishi?"
19Wakunga wakamwambia Farao, "Wanawake wa Kiebrania si kama wanawake wa Kimisri—wana nguvu, huzaa kabla ya mkunga kuwafikia."
20Basi Baba yetu akawatendea mema wale wakunga, na watu wakaongezeka na kuwa hodari sana. 21Na kwa sababu wakunga walimcha Baba yetu, akawapa jamaa zao wenyewe. 22Kisha Farao akawaamuru watu wake wote, "Kila mtoto wa kiume atakayezaliwa kwa Waebrania mtupeni katika Mto Nile, lakini kila mtoto wa kike mwacheni aishi."