Kuvitunza Vitu Anavyopoteza Ndugu Yako
22 1Usimwone ng'ombe au kondoo wa ndugu yako akipotea njiani halafu ujifanye hukuona; hakika umrudishe kwa ndugu yako. 2Kama ndugu yako hayuko karibu, au humfahamu, uilete nyumbani kwako na uitunze mpaka atakapoiuliza, kisha umrudishie. 3Fanya vivyo hivyo kwa punda wake, vivyo hivyo kwa vazi lake, na vivyo hivyo kwa kila kitu ndugu yako akipotezacho nawe ukakikuta; huna ruhusa ya kujifanya hukuona. 4Usimwone punda wa ndugu yako au ng'ombe wake ameanguka njiani halafu ujifanye hukuona; hakika umsaidie kumwinua.
5Mwanamke asivae mavazi ya mwanamume, wala mwanamume asivae mavazi ya mwanamke, kwa maana kila afanyaye mambo haya ni chukizo kwa Baba yako.
6Ukikutana na kioto cha ndege njiani, katika mti wowote au juu ya ardhi, chenye makinda au mayai, na mama ameatamia makinda au mayai, usimchukue mama pamoja na makinda. 7Hakika umwache mama aende zake, lakini uyachukue makinda kwa ajili yako, ili upate heri na siku zako ziwe nyingi.
8Ujengapo nyumba mpya, weka ukingo juu ya dari yake, ili nyumba yako isije ikawa na hatia ya damu mtu akianguka kutoka humo.
9Usipande shamba lako la mizabibu kwa mbegu za aina mbili, ili mavuno yote—mbegu uliyoipanda na matunda ya shamba la mizabibu—yasije yakachukuliwa. 10Usilime kwa ng'ombe na punda waliofungwa nira pamoja. 11Usivae nguo iliyofumwa kwa sufu na kitani pamoja.
12Weka vishada katika pembe nne za vazi ulivaalo.
Kuliheshimu Agano la Ndoa
13Mtu akioa mke, kisha baada ya kulala naye akaanza kumchukia, 14na akamshtaki kwa tabia ya aibu, akimwharibia jina, akisema, "Nilimwoa mwanamke huyu, lakini nilipomkaribia sikupata uthibitisho wa ubikira wake," 15ndipo baba na mama wa yule mwanamwali watakapochukua na kuutoa uthibitisho wa ubikira wake mbele ya wazee wa mji langoni. 16Baba wa yule mwanamwali atawaambia wazee, "Nilimtoa binti yangu kwa mtu huyu awe mke wake, naye anamchukia. 17Sasa amemshtaki kwa tabia ya aibu, akisema, 'Sikupata uthibitisho wa ubikira wa binti yako.' Lakini huu hapa uthibitisho wa ubikira wa binti yangu." Nao wataitandaza nguo mbele ya wazee wa mji. 18Ndipo wazee wa mji ule watakapomchukua mtu yule na kumrudi, 19nao watamtoza faini ya vipande vya fedha kama ujira wa mwaka mzima, na kumpa baba wa yule mwanamwali, kwa sababu amemwaribia jina bikira wa Israeli. Naye atabaki kuwa mke wake; hana ruhusa ya kumwacha siku zote za maisha yake.
20Lakini kama shtaka ni la kweli, na uthibitisho wa ubikira wa yule mwanamwali haukupatikana, 21watamleta yule mwanamwali mlangoni pa nyumba ya baba yake, na watu wa mji wake watampiga mawe hata afe kwa kufanya jambo la aibu katika Israeli—kufanya uzinzi katika nyumba ya baba yake. Ondoa uovu kati yenu.
22Mtu akikutwa amelala na mke wa mtu mwingine, wote wawili watakufa—mwanamume aliyelala naye, na yule mwanamke. Ondoa uovu katika Israeli. 23Kama mwanamwali, bikira aliyeposwa na mtu, na mwanamume mwingine akamkuta mjini na kulala naye, 24waleteni wote wawili langoni pa mji ule na kuwapiga mawe hata wafe: yule mwanamwali, kwa sababu hakupiga kelele za kuomba msaada mjini; na yule mwanamume, kwa sababu alimtenda dhuluma mke wa jirani yake. Ondoa uovu kati yenu. 25Lakini kama mwanamume atamkuta yule mwanamwali aliyeposwa kondeni, akamshika na kulala naye, yeye peke yake ndiye atakayekufa. 26Msimfanye lolote yule mwanamwali; hana dhambi inayostahili kifo. Jambo hili ni kama mtu amshambuliaye jirani yake na kumwua: 27kwa maana alimkuta kondeni; yule mwanamwali aliyeposwa alipiga kelele, lakini hakuwako wa kumwokoa. 28Kama mwanamume atamkuta mwanamwali bikira ambaye hajaposwa, akamshika, akalala naye, nao wakagunduliwa, 29yule mwanamume aliyelala naye atampa baba wa mwanamwali vipande vya fedha kama ujira wa nusu mwaka; naye atakuwa mke wake kwa sababu alimtenda dhuluma, wala hana ruhusa ya kumwacha maisha yake yote. 30Mtu asimwoe mke wa baba yake; asiliaibishe kitanda cha ndoa cha baba yake.