Baba Yetu Aongeza Mafuta ya Mjane
4 1Mke wa mmoja wa wana wa manabii akamlilia Elisha, akisema, "Mtumishi wako, mume wangu, amekufa, nawe unajua ya kuwa mtumishi wako alimcha Baba yetu. Sasa mdai amekuja kuwachukua wanangu wawili wawe watumwa."
2Elisha akamwuliza, "Nikufanyie nini? Niambie, una nini nyumbani mwako?" Akasema, "Mtumishi wako hana kitu nyumbani ila chupa ya mafuta."
3Ndipo akasema, "Nenda, uazime vyombo huko nje kutoka kwa majirani zako wote—vyombo vitupu, wala visiwe vichache. 4Kisha ingia ndani, ufunge mlango nyuma yako na wanao, ukamimine mafuta ndani ya vyombo hivi vyote. Kila kimoja kikijaa, kiweke kando."
5Basi akaondoka kwake, akafunga mlango nyuma yake na wanawe; wakawa wakimletea vyombo, naye akawa akimimina. 6Vyombo vilipojaa, akamwambia mwanawe, "Niletee chombo kingine." Akamwambia, "Hakuna kingine kilichobaki." Ndipo mafuta yakakoma.
7Akaja akamwambia mtu wa Baba yetu, naye akasema, "Nenda, uyauze mafuta, ulipe deni lako, nawe na wanao mwishi kwa hayo yaliyobaki."
Ahadi ya Baba kwa Mwanamke wa Shunemu
8Siku moja Elisha akapita kati ya Shunemu, palipokuwa na mwanamke tajiri; naye akamsihi ale chakula. Basi kila alipopita, akaingia humo kula chakula. 9Akamwambia mumewe, "Tazama, najua ya kuwa mtu huyu apitaye kwetu mara kwa mara ni mtu mtakatifu wa Baba yetu. 10Tafadhali na tumfanyie chumba kidogo juu ya dari, tuweke humo kitanda, na meza, na kiti, na taa, ili awezapo kuja atwae humo."
11Siku moja Elisha akaja huko, akaingia katika kile chumba cha juu, akalala humo. 12Akamwambia Gehazi, mtumishi wake, "Mwite huyu mwanamke wa Shunemu." Akamwita, naye akasimama mbele yake. 13Elisha akamwambia Gehazi, "Mwambie: Umejitaabisha kwa ajili yetu kwa taabu hii yote. Sasa nikufanyie nini? Je, kuna neno unalotaka niseme kwa niaba yako kwa mfalme au kwa jemadari wa jeshi?" Akajibu, "Nakaa kati ya watu wangu."
14Elisha akauliza, "Basi, amfanyiwe nini?" Gehazi akasema, "Kweli, huyu hana mwana, na mumewe ni mzee."
15Akasema, "Mwite." Basi akamwita, naye akasimama mlangoni. 16Akasema, "Wakati kama huu, mwakani, utamkumbatia mwana." Akasema, "La, bwana wangu, wewe mtu wa Baba yetu, usimdanganye mtumishi wako."
17Yule mwanamke akapata mimba, akazaa mwana wakati ule ule mwaka uliofuata, kama Elisha alivyomwambia.
18Yule mtoto akakua; siku moja akatoka kwenda kwa babaye, kwa wavunaji. 19Akamwambia babaye, "Kichwa changu! Kichwa changu!" Naye babaye akamwambia mtumishi, "Mchukue, umpeleke kwa mamaye."
20Akamchukua, akampeleka kwa mamaye; yule mtoto akakaa magotini pake hata adhuhuri, ndipo akafa. 21Basi akapanda, akamlaza juu ya kitanda cha yule mtu wa Baba yetu, akamfungia mlango, akatoka. 22Akamwita mumewe, akasema, "Tafadhali niletee mtumishi mmoja na punda mmoja, ili nikimbie kwa mtu wa Baba yetu, kisha nirudi."
23Akauliza, "Kwa nini kwenda kwake leo? Si mwandamo wa mwezi wala si Sabato." Akasema, "Ni salama tu."
24Ndipo akatandika punda, akamwambia mtumishi wake, "Endesha, uende mbele; wala usinilegeze mwendo isipokuwa nikuambie." 25Basi akaondoka, akamwendea yule mtu wa Baba yetu katika mlima Karmeli. Ikawa yule mtu wa Baba yetu alipomwona kwa mbali, akamwambia Gehazi, mtumishi wake, "Tazama, huyu ni yule mwanamke wa Shunemu. 26Sasa, tafadhali mbilie umlaki, umwulize, 'Je, u salama? Mumeo ni salama? Mtoto ni salama?'" Akajibu, "Ni salama."
27Alipomfikia yule mtu wa Baba yetu mlimani, akamshika miguu. Gehazi akakaribia amsukume, lakini yule mtu wa Baba yetu akasema, "Mwache; kwa maana nafsi yake ina uchungu ndani yake, na Baba yetu amenificha jambo hili, wala hakuniambia."
28Ndipo akasema, "Je, mimi nilikuomba bwana wangu mwana? Sikusema, 'Usinipe matumaini ya bure'?"
29Elisha akamwambia Gehazi, "Jikaze viuno vyako, uichukue fimbo yangu mkononi mwako, uende zako. Ukikutana na mtu ye yote, usimsalimu; na mtu akikusalimu, usimjibu. Kisha uilaze fimbo yangu juu ya uso wa yule mtoto."
30Lakini mama yake yule mtoto akasema, "Kama Baba yetu aishivyo, na kama wewe uishivyo, sitakuacha." Basi akaondoka, akamfuata.
31Gehazi akatangulia mbele yao, akaiweka ile fimbo juu ya uso wa yule mtoto, lakini hapakuwa na sauti wala jibu. Kwa hiyo akarudi kumlaki Elisha, akamwambia, "Yule mtoto hakuamka."
32Elisha alipoingia nyumbani, tazama, yule mtoto amekufa, amelazwa juu ya kitanda chake. 33Basi akaingia ndani, akajifungia mlango wao wawili, akamwomba Baba yetu. 34Kisha akapanda kitandani, akajilaza juu ya yule mtoto—kinywa chake juu ya kinywa chake, na macho yake juu ya macho yake, na mikono yake juu ya mikono yake. Alipojinyoosha juu yake, mwili wa yule mtoto ukapata joto. 35Ndipo akashuka, akatembea humo chumbani mara moja huko na huko, kisha akapanda tena, akajinyoosha juu ya yule mtoto. Yule mtoto akapiga chafya mara saba, akafumbua macho yake. 36Elisha akamwita Gehazi, akasema, "Mwite huyu mwanamke wa Shunemu." Basi akamwita; naye alipomjia, akamwambia, "Mchukue mwanao."
37Akaingia, akaanguka miguuni pake, akainama hata nchi, kisha akamchukua mwanawe, akatoka.
Baba Aponya Mchuzi wa Kifo
38Elisha akarudi Gilgali wakati wa njaa katika nchi. Nao wana wa manabii walipokuwa wameketi mbele yake, akamwambia mtumishi wake, "Teleka sufuria kubwa jikoni, uwapikie wana wa manabii mchuzi."
39Mmoja akatoka kwenda shambani ili achume mboga, akaona mtango-mwitu, akachuma humo matango-mwitu, akajaza nguo yake, akarudi, akayakatakata na kuyatia katika ile sufuria ya mchuzi—maana hawakuyajua yalikuwa nini. 40Basi wakawapakulia watu wale ili wale. Ikawa walipoula ule mchuzi, wakapiga kelele, wakisema, "Ee mtu wa Baba yetu, mna mauti ndani ya sufuria!" Wala hawakuweza kuula.
41Akasema, "Basi leteni unga." Akautia katika ile sufuria, akasema, "Wapakulieni watu ili wale." Wala hapakuwa na neno lo lote la kudhuru ndani ya sufuria.
42Akaja mtu mmoja kutoka Baal-shalisha, akamletea yule mtu wa Baba yetu mkate wa malimbuko—mikate ishirini ya shayiri, na masuke ya nafaka mpya katika mfuko wake. Naye Elisha akasema, "Wape watu, wale."
43Mtumishi wake akasema, "Je, niweke kiasi hiki mbele ya watu mia moja?" Lakini akasema tena, "Wape watu, wale; kwa maana Baba yetu asema hivi: Watakula, na kusaza."
44Basi akaweka mbele yao, wakala, na kusaza, sawasawa na neno la Baba yetu.